Ticker

6/recent/ticker-posts

AKATWA MGUU NA MAMBA AKISAFISHA UTUMBO WA NGURUWE MTONI

 

Paulo Mapunda (54) mkazi wa kijiji cha Kipingu kata ya Ruhuhu Wilayani Ludewa mkoani Njombe amenusurika kifo baada ya kuvamiwa na Mamba wakati akisafisha utumbo wa Nguruwe kandokando ya mto Ruhuhu na kumkata mguu wake wa kulia katika eneo la goti.


Akizungumza akiwa katika hospitali ya Peramiho mkoani Ruvuma majeruhi huyo amesema majira ya saa tano asubuhi siku ya jumapili  01, 2023 nyumbani kwake kulikuwa na sherehe ya kipaimara hivyo walichinja Nguruwe ambapo yeye alichukua utumbo kwenda kuusafisha mtoni hapo huku akiwa ndani ya mtumbwi ndipo Mamba huyo alijitokeza na kubinua mtumbwi kisha yeye kuangukia ndani ya maji.


Amesema Mamba huyo alimkamata mguu wake wa kulia na kumzamisha kwenye maji lakini alijitahidi kuushikilia mtumbwi huku wakivutana na Mamba huku akipiga kelele za kuomba msaada na watu walipojitokeza ndipo mamba huyo akamkata mguu wake na kuondoka nao ndipo akaokolewa na kukimbizwa hospitali ya Peramiho.


Ameongeza kuwa mpaka sasa tayari amekwishapata matibabu ya awali na anatakiwa kufanyiwa operesheni lakini anashindwa kupata huduma hiyo kutokana na kutokuwa na fedha za kulipia matibabu hayo huku akiiangukia serikali kuwaletea mabomba ya maji kwani mara kwa mara watu wamekuwa wakijeruhiwa na Mamba huku wengine wakiuawa kutokana na wananchi wa maeneo hayo kutegemea zaidi maji ya mto huo.


Aidha kwa upande wake mtendaji wa kata hiyo Yusuph Lukuwi amethibitisha kutokea kwa tukio hilo huku mwenyekiti wa kijiji cha Kipingu Alponce Mbeya akisema baada ya tukio hilo kutokea walikopa fedha mahali kiasi cha sh.700,000 kwa ajili ya gari la wagonjwa na matibabu ya awali na bado hazikutosheleza hivyo bado kuna uhitaji wa fedha zaidi kwa ajili ya matibabu hayo.

Post a Comment

0 Comments