" SHUWASA YAJIPANGA UJENZI WA MRADI WA KUCHAKATA MAJITAKA MWAKA HUU WANANCHI KUNUFAIKA

SHUWASA YAJIPANGA UJENZI WA MRADI WA KUCHAKATA MAJITAKA MWAKA HUU WANANCHI KUNUFAIKA

Na Mapuli Misalaba, Shinyanga

Mkurugenzi mtendaji wa Mamlaka ya majisafi na usafi wa mazingira Shinyanga (SHUWASA)  Mhandisi Yusuph Katopola amesema fedha zaidi ya Milioni Mia saba zitatumika katika ujenzi wa mradi wa kuchakata majitaka ili kufikia mita za ujazo mia moja (100) kwa siku ambapo mamlaka hiyo kwa sasa inauwezo wa kutibu majitaka kwa mita za ujazo 40.

Ameyasema hayo wakati akitoa taarifa ya utekelezaji wa majukumu ya mamlaka hiyo kwa waandishi wa habari ambapo amesema kupitia mradi wa IFF – OBA, SHUWASA itatekeleza ujenzi wa mradi wa kuchakata majitaka ikiwa lengo ni kufikia mita za ujazo mia moja na kwamba mamlaka hiyo kwa sasa ipo kwenye hatua ya ununuzi wa Gari la majitaka kama sehemu ya usimamizi wa mazingira.

Aidha Mkurugenzi mtendaji wa SHUWASA  Mhandisi Yusuph Katopola amesema serikali ya Tanzania kupitia Wizara ya fedha ilisaini mkataba wa fedha na shirika la maendeleo la Ufaransa (French Development Agency – AFD) kwa ajili ya ujenzi wa mradi wa majisafi na usafi wa mazingira kwa eneo linalohudumiwa na SHUWASA.

Ameeleza kuwa mkataba huo wenye thamani ya Euro Milioni 76 ni mkopo wa riba nafuu kutoka shirika la maendeleo la Ufaransa na Euro ambapo Milioni moja zitatolewa na serikali ya Tanzania na kwamba mkataba huo ulisainiwa Juni 20,2022 na unatarajiwa kuanza rasmi Mwezi Mei Mwaka huu 2024 huku ukitarajiwa kukamilika Mwezi Mei Mwaka 2028.

Mhandisi Katopola amesema SHUWASA inaendelea na utekelezaji wa mradi huo ambao unahusisha shughuli mbalimbali ikiwemo ujenzi wa mtandao wa majisafi kwa kilomita 298, ukarabati wa mtandao chakavu wa maji safi kwa takribani kilomita mia moja (100) pamoja na ujenzi wa matenki mawili ya kuhifadhi majisafi.

SHUWASA tunaendelea na utekelezaji wa mradi huu ambao unahusisha kazi mbalimbali ikiwemo ujenzi wa matenki mawili ya kuhifadhia majisafi yenye uwezo wa kuhifadhi mita mita za ujazo Elfu moja mia tano (1,500) eneo la Kolandoto na mita za ujazo 250 eneo la Didia, kuna kazi ya ujenzi wa mitambo minne ya kuchakata tope kinyesi eneo la Ihapa na Mwagala kwa Manispaa ya Shinyanga lakini pia Kituli na Iselamagazi Halmashauri ya Manispaa ya Shinyanga, kazi nyingine ni ukarabati wa mtambo wa kutibu maji Ning’hwa na tathimini ya ufanisi na ukarabati wa bwawa la Ning’hwa, lakini pia kuna kazi ya kuijengea uwezo taasisi ikiwa ni pamoja na ujenzi wa jingo jipya la ofisi ya SHUWASA”.amesema Mhandisi Katopola.

SHUWASA imeshatangaza zabuni mbili za kupata wahandisi washauri kwa eneo la ujenzi na usimamizi (Design & Supervision) pamoja na eneo la usaidizi kwa mamlaka (Technical Assistance) kwa usimamizi wa mradi na zabuni moja ya kandarasi ya ujenzi (Construction of portable water infrastructure) ambazo zipo katika hatua mbalimbali za utekelezaji”.amesema Mkurugnzi mtendaji SHUWASA

Mkurugenzi mtendaji wa Mamlaka ya majisafi na usafi wa mazingira Shinyanga (SHUWASA)  amesema mamlaka hiyo inaendelea na zoezi la kurasimisha maeneo mbalimbali ya mradi ambapo maombi ya fedha za fidia kwa waathirika wa mradi yamewasilishwa Wizara ya Maji Oktoba 24, 2023 kwa ajili ya hatua zaidi za utekelezaji.

Amesema kwa sasa SHUWASA inaendelea na maandalizi ya nyaraka mbalimbali kutoka kwa mfadhili na taasisi nyingine za serikali ili kuwezesha mikataba ya shughuli za ujenzi kusainiwa na utekelezaji uweze kuanza.

Inatarajiwa kuwa mkandarasi atakabidhiwa eneo la mradi na kuanza shughuli za ujenzi Mwezi Machi Mwaka huu 2024 ambapo mradi utahusisha ujenzi wa vyoo vya kisasa katika maeneo ya kijamii ikiwemo shule, kituo cha afya pamoja na stendi vipatavyo 36.

Mamlaka ya majisafi na usafi wa mazingira Shinyanga (SHUWASA) inajihusisha na utoaji wa huduma ya majisafi na usafi wa mazingira katika Halmashauri ya Manispaa ya Shinyanga na miji midogo ta Tinde, Didia na Iselamagazi iliyopo Halmashauri ya Wilaya ya Shinyanga.

Mkurugenzi mtendaji wa Mamlaka ya majisafi na usafi wa mazingira Shinyanga (SHUWASA)  Mhandisi Yusuph Katopola akizungumza ambapo upande wa kulia ni afisa mahusiano na mawasiliano SHUWASA Nsianel Gerald akiandika maswali yanayoulizwa na waandishi wa habari. 


Post a Comment

Previous Post Next Post