Ticker

6/recent/ticker-posts

SALOME MAKAMBA CUP YAFIKIA HATUA YA ROBO FAINALI

 

Na Elisha Petro

Timu Sita kati ya 12 zilizotinga hatua ya pili katika michuano ya Salome Makamba Cup inayoendelea sehemu mbalimbali za Manisapa ya Shinyanga, zimefanikiwa kutinga hatua ya robo fainali ya mashindano hayo, yaliyoanza kurindima wiki moja iliyopita.

Timu hizo ni Mwagala FC kutoka Kata ya Kolandoto, Bugweto FC ya Kata ya Ibadakuli, Boko FC ya Kata ya Ndembezi, Ngokolo Stars ya Kata ya Ngokolo, Shy Veteran FC ya Kata ya Kambarage na Chipukizi FC ya Kata ya Ngokolo.

Timu hizo zimefanikiwa kutinga hatua ya robo fainali katika michuano hiyo baada ya kupata ushindi katika michezo yao ya hatua ya pili na kukamilisha timu sita zilizofuzu hatua ya tatu (robo fainali) ambazo zitamenyana ili kuwapata washindi watatu ambao wataungana na timu moja kutoka ya mshindwa bora (best loser) kuingia hatua ya nusu Fainali ya mashindano hayo.

Bugweto FC wamefanikiwa kutinga hatua ya robo fainali kwa mikwaju ya Penati 3 – 2 dhidi ya Mwadui United FC ambapo Chipukizi FC walipata ushindi wa goli 1 – 0 dhidi ya Home boys FC na kupata tiketi ya kufuzu hatua ya robo fainali.

Timu nyingine ni Mwagala FC waliofuzu kwa mikwaju ya Panati 3 – 2 kufuatia sare ya goli 1 – 1 dhidi ya timu ya Mchicha FC.

Wakati huohuo, Ngokolo FC wamefanikiwa kutinga hatua ya robo fainali licha ya kichapo cha goli 2 – 1 baada ya Town Stars kuchezesha wachezaji waliotumika katika timu nyingine ambazo tayari zimeshaondolewa katika michuano hiyo, wachezaji hao ni David Buma[Cheu], Fude, Nyanzu na aliyekuwaa  nahodha wa timu ya Ngalya FC katika mchezo uliowakutanisha  Ngalya FC dhidi ya  Boko FC.

Boko FC wametinga hatua ya robo fainali baada ya ushindi wa goli 2 – 0 dhidi ya Katunda FC ambapo Shy Veteran FC wamefanikiwa kupata ushindi wa goli 2 – 1 dhidi ya Magereza FC katika mchezo uliochezwa kwenye uwanja wa Sabasaba .

Leo Jumatatu ya tarehe 27.05.2024 hatua ya nusu fainali itaanza kurindima kuanzia majira ya saa 10:00 jioni kwa wenyeji Bugweto FC kuwakaribisha jirani zao Mwagala FC katika uwanja wa Bugweto.

Michuano hiyo inadhaminiwa na Mbunge wa viti maalumu Mkoa wa Shinyanga Mh. Salome Makamba ambapo zawadi za washindi zitakabidhiwa Jumamosi ya tarehe 01.06.2024 katika uwanja wa Sabasaba uliopo Kambarage mjini Shinyanga, baada ya mchezo wa fainali kumalizika.

Wachezaji wa timu ya Ngokolo Stars wakiwa kwenye picha ya pamoja kabla ya mchezo dhidi ya Town Stars katika uwanja wa Boko uliopo kata ya Ndembezi

Wachezaji wa timu ya Town Stars wakiwa kwenye picha ya pamoja kabla ya mchezo dhidi ya Ngokolo Stars katika uwanja wa Boko uliopo kata ya Ndembezi

Timu zote mbili (Town Stars na Ngokolo Stars ) zikipokea maelekezo kabla ya mchezo kuanza

Mwamuzi akiwakagua wachezaji wa timu zote zote mbili

Wachezaji wa Ngolo Stars na Town Stars wakisalimiana kabla ya mchezo

Picha za matukio mbalimbali wakati wa mchezo ulowakutanisha Town Stars vs Ngokolo Stars katika uwanja wa Boko

Benchi la ufundi la timu ya Ngokolo Stars pembeni yao (kulia) ni baadhi ya mashabiki waliojitokeza kushuhudia mchezo

Mashabiki wakiendelea kupata burudani wakati wa mchezo

Mchezo wa pili ukiendelea kati ya Katunda FC dhidi ya Boko FC katika uwanja wa Veta Shinyanga

Waamuzi wakiwa katika picha ya pamoja kabla ya mchezo kuanza kati ya SHY Veteran FC dhidi ya Magereza FC

Kikosi cha SHY Veteran FC katika picha ya pamoja kabla ya mchezo kuanza dhidi ya Magereza FC

Kikosi cha Magereza FC kabla ya mchezo kuanza

Viongozi wa timu zote mbili (SHY Veteran FC na Magereza FC) wakipewa maelekezo kabla ya mchezo kuanza

Marefaree na Viongozi wa timu wakiwa katika picha ya pamoja kabla ya mchezo kuanza

Picha za matukio mbalimbali wakati mchezo ukiendelea

Baadhi ya Mashabiki wakiendelea kupata burudani katika uwanja wa SabaSaba

Post a Comment

0 Comments