Ticker

6/recent/ticker-posts

SERIKALI KUENDELEA NA UCHUNGUZI BAADA YA KULIFUNGA KANISA LA CHURCH OF GOD NA KUMZUIA MCHUNGAJI MUSSA KUFIKA KATIKA KIJIJI CHA MENDO

Na Mapuli Kitina Misalaba

Mkuu wa wilaya ya Shinyanga Wakili Julius Mtatiro amezuia kuendelea kwa huduma za ibada katika kanisa la "Church of God" lililopo Kijiji cha Mendo kata ya Ilola Halmashauri ya Shinyanga kwa tuhuma za Mchungaji wa kanisa hilo kuwazuia Waumini wake kwenda kujifungua katika kituo cha afya.

Hatua hiyo imefikiwa ikiwa ni siku kadhaa tangu kutokea kwa tukio la Mwanamke mmoja aliyejulikana kwa jina la Neema Juma kuzalishwa Kanisani na wahudumu wa Kanisa hilo hali iliyosababisha mtoto kupoteza maisha.

DC Mtatiro pamoja na mambo mengine amemzuia mchungaji Endrew Charles Mussa wa kanisa hilo la Church of God kufika katika kijiji cha Mendo mpaka pale uchunguzi utakapokamilika na kupewa taarifa.

“Wakiti tunaendelea na hili jambo, hii Nyumba ya ibada ninaifunga kuanzia leo siwezi nikawa na Nyumba ya ibada kwenye Wilaya yangu inaendesha kazi za kuwazalisha akina Mama, inawakataza waziende kliniki inawalazimisha kuwazalisha ndani ya hiyo Nyumba kwahiyo tunaifunga rasmi halafu tutaendelea na taratibu zingine baada ya kuwa tumeifunga na hakutakuwa na mamlaka nyingine yoyote itakayopaswa kuja kuifungua aidha ni mamlaka yangu au mamlaka ya juu yangu kwahiyo asije akajitokeza mtu mwingine yoyote akaingilia jambo hili tutamchukulia hatua kali na kwa sababu hiyo hakuna tena mtu anaruhusiwa kuingia tena humo ndani ya NYumba ya Kanisa hili ili tufanye uchunguzi wa masuala mbalimbali ambayo yamebakia”.

“Lakini pia Mchungaji Endrew wakati uchunguzi huu unaendelea na mpaka utakapopewa taarifa usikanyage kwenye kijiji cha Mendo kuanzia leo kwahiyo utakapotoka hapa usikanyage tena kwenye hiki kijiji fanya shughuli zako sehemu zingine hapa usikanyage ili tuendelee na uchunguzi”.

“Jambo la tatu hii Nyumba ya ibada nimeambiwa iliwahi kuanguka upande mmoja ikanyanyuliwa kwahiyo katibu tawala we unda timu yako ipitie maana hii Nyumba ya ibada ni Nyumba ya umma inautaratibu wa ujenzi wake kwahiyo katibu tawala unda timu iwe na mainginia wa Mkoa, mainjinia wa Wilaya, weka timu ya TAKUKURU na vyombo vingine na wataalamu wa Halmashauri kwahiyo unda timu kama ya watu saba waje wafanye utaratibu wote ili tujiridhisha, tujue tofali zilizoweka hapa zimepimwa kwa mujibu wa sheria kwahiyo kama havikufuata utaratibu jengo itabidi libaki kama bagare”amesema DC Mtatiro

Mkuu wa Wilaya ya Shinyanga Wakili Julius Mtatiro pia amemuagiza afisa utumishi wa Halmashauri ya Wilaya ya Shinyanga, kumuondoa kwenye kijiji cha Mendo mtendaji wa kijiji hicho Bi. Christina Mgeni ambapo DC Mtatiro amesisitiza mtendaji huyo apangiwe majukumu yake kwenye kijiji kingine na siyo tarafa hiyo.

Awali DC Mtatiro kabla ya kuchukua maamuzi hayo ametoa nafasi ya kumsikiliza kila mtu katika mkutano huo wa hadhara ambapo wakazi wa kijiji cha Mendo wameeleza mambo mbalimbali yanayosadikika kufanyika katika kanisa hilo la Church of God.

Wakazi wa kijiji hicho wamesema kilifanyika kikao cha kijiji ambapo kwa pamoja waliazimia kuwa hawataka kuona huduma zikiendelea katika kanisa hilo ambapo waliiomba serikali kulifunga kanisa hilo pamoja na mchungaji ili kuepusha athari zaidi kwa wananchi.

Wananchi hao wameeleza kuwa mchungaji Mussa aliwahi kuwazuia waumini wa kanisa hilo kuwa wasifanye shughuli za kilimo Mwezi wa kumi na moja na kumi na mbili 2024 ambaye aliwaambiwa kuwa maji hayo siyo ya baraka na kwamba waanze kulima  Mwezi wa kwanza 2024 ambapo imeelezwa kuwa baada ya waumini wao kuanza kulima Mwezi wa kwanza hawajafanikiwa kuvuna chochote.

Wananchi hao pia wamesema watoto wa wazazi wanaosali katika kanisa hilo wameshazuiliwa kuhudhuria kwenye chanjo zote za serikali  lakini pia imeelezwa kuwa waumini wa kanisa hilo wamezuiliwa kuwaita majina ya ukoo watoto wao.

Pia wananchi hao wamesema akina Mama wanaosali katika kanisa hilo wamezuiliwa kuhudhurika kliniki zao pamoja na kliniki za watoto chini ya umuri wa Miaka mitano.

Wakazi wa kijiji hicho wameendelea kusema kuwa toka awali walilikataa jengo la kanisa hilo ambapo wamesema jengo hilo limejengwa kwa kiwango cha chini na kwamba limewahi kudondoka upande mmoja, likaunganishwa ili ibada ziendelee kwahiyo wamehofia usalama wa waumini wa kanisa hilo.

Wananchi wamesema kanisa hilo limesababisha vifo vya watu takribani wane kwa nyakati tofauti ambapo wamezitaka mamlaka husika kuchukua hatua za kisheria kwa mchungaji wa kanisa hilo ili iwe fundisho na kwa watu wengine.

Hata hivyo Mchungaji Endrew Charles Mussa wa kanisa hilo la Church of God baada ya kuulizwa ameyakana madai yote ya wananchi kuwa siyo kweli.

Aidha pamoja na mambo mengine wananchi wa kijiji hicho wameeleza kuwa  kanisa hilo la Church of God limekuwa likiendesha ibada zake kuanzia saa nane mchana hadi saa nne usiku na ibada nyingine ni kuanzia saa kumi usiku hadi saa mbili asubuhi na kwamba jambo hilo limekuwa ni kero kwa wakazi wa kijiji cha Mendo kata ya Ilola Halmashauri ya Wilaya ya Shinyanga.

Mkuu wa Wilaya ya Shinyanga Wakili Julius Mtatiro akizungumza.

 

Post a Comment

0 Comments