DED KASULU ATEKELEZA AGIZO LA MAKAMU WA RAIS

 Na Respice Swetu, Kasulu

Ikiwa ni siku moja baada ya Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dr. Philip Isidor Mpango kutoa agizo kwa mkurugenzi mtendaji wa halmashauri ya wilaya ya Kasulu kufanya mkutano na wakazi wa kijiji cha Nyakitonto kilichopo kwenye halmashauri hiyo, agizo hilo limetekelezwa.

Kufuatia agizo hilo, mkurugenzi wa halmashauri ya wilaya ya Kasulu Dr. Mashimba akifuatana na wataalamu kutoka katika ofisi yake, amezungumza na wakazi wa kijiji cha Nyakitonto katika mkutano wa hadhara uliofanyika kijijini hapo.

Katika mkutano huo wakazi wa kata ya Nyakitonto wakiongozwa na diwani wa kata hiyo Daniel Nzababa, pamoja na kupata fursa ya kufahamiana na mkurugenzi mtendaji wa halmashauri ya wilaya ya Kasulu, waliutumia mkutano huo pia kuwasilisha hoja mbalimbali za kujiletea maendeleo.

Miongoni mwa hoja zilizowasilishwa katika mkutano huo ni pamoja na zilizohusu ardhi, huduma za afya, huduma za maji, huduma elimu, kilimo, hifadhi ya mazingira, miundombinu na ushirikishwaji.

Akijibu hoja hizo Dr. Mashimba ambaye amehamia katika halmashauri ya wilaya ya Kasulu hivi karibuni kutoka katika halmashauri ya wilaya ya Chamwino iliyopo mkoani Dodoma amesema, lengo lake ni kuiona Nyakitonto na halmashauri nzima ya wilaya ya Kasulu inapata maendeleo.

Ili kuyafikia maendeleo hayo Dr. Mashimba amesema, hatua mbalimbali zinapaswa kuchukuliwa.

Dr. Mashimba amezitaja hatua hizo kuwa ni pamoja na kutenga maeneo yatakayotumika kwa ajili ya kujenga viwanda na taasisi mbalimbali kama mabenki, TRA, maduka, sehemu ya kuegesha malori na kituo cha biashara.

Dr. Mashimba amewatahadharisha wakazi wa halmashauri ya wilaya ya Kasulu kuwa katika kuyafikia maendeo hayo kuna gharama.

Amezitaja baadhi ya gharama hizo kuwa ni pamoja na kutoa ardhi kwa ajili ya upitishaji wa miundombinu ya barabara, maji na kuchangia zoezi la urasimishaji na mpango bora wa matumizi ardhi.

Pamoja na mkutano huo kufanyika kutokana na maagizo ya Makamu wa Rais, tangu kufika kwake Dr. Mashimba  amekwisha fanya ziara katika vijiji na kata mbalimbali za halmashauri ya wilaya ya Kasulu  kwa lengo la kagua miradi ya maendeleo na kuzungumza na wananchi.

 

TAZAMA VIDEO
Previous Post Next Post