Ticker

6/recent/ticker-posts

MADIWANI VITI MAALUM HALMASHAURI YA WILAYA YA SHINYANGA WATAJA NJIA ZA KUTOKOMEZA UKATILI KATIKA JAMII

 

Na Mapuli Kitina Misalaba

Madiwani wa viti maalum Halmashauri ya Wilaya ya Shinyanga wamewahimiza wazazi, walezi na jamii kuwalea watoto katika maadili mema na misingi inayozingatia mila na desturi za eneo husika ili kuepukana na vitendo vya ukatili ikiwemo ubakaji na ulawiti kwa watoto.

 Wameyasema hayo leo Alhamisi Julai 11,2024 katika ziara yao kata ya Nyabusalu pamoja na kata ya Iselamagazi ambapo wameendelea na ziara yao kwa lengo la kuhamasisha wanawake na wanachama wote wa CCM na jumuiya zake kujitokeza kujiandikisha kwenye daftari la kudumu la wapiga kura, kuhamasisha wanawake kujitokeza kuchukua fomu za kugombea nafasi mbalimbali za uongozi, Usajili wa wanachama wa CCM na jumuiya zake pamoja na na kukemea Ukatili wa kijinsia.

Akizungumza Mwenyekiti wa madiwani viti maalum Halmashauri ya Wilaya ya Shinyanga ambaye ni diwani wa viti maalum kata ya Lyabukande Mhe. Zawadi Lufungulo Mwasha amewasisitiza wazazi na walezi kusimamia maadili kwa watoto huku akiwaomba viongozi wa dini kuendelea kukemea mmomonyoko wa maadili.

“Ukatili nimegundua kwamba ni malezi yanapungua yaani maadili yetu ya kitanzania yamepolomoka sana motto usipomlea vizuri huyo ndiye atakuwa mbakaji, atakuwa mlawiti, atakuwa shoga u nakuta motto amevaa mtepesho na wewe mama unaangalia tu na wewe baba unaangalia tu ebu turudi kabisa kwenye maadili yetu tuwe wakali watoto hawa tuwakemee kizazi chetu kimaharibika sana, hivyo hivyo viongozi wa dini msaidie hili semeni makanisani semeni kwenye miskiti ili haya maadili tuendane na mila zetu za kitanzania”.amesema Mhe. Zawadi

Aidha Mhe. Zawadi pamoja na mambo mengine ameendelea kumpongeza  Rais wa Jamhuri ya Muungani wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan pamoja na Mbunge wa jimbo la Solwa Mhe. Ahmed Salum kwa kuendelea kuwahudumia wananchi kwa weledi katika utekelezaji wa majukumu yao kwa kuzingatia  katiba ya Chama cha Mapinduzi CCM.

Pia madiwani hao wamempongeza diwani wa kata ya Lyabusalu kwa usimamizi mzuri wa miradi ya maendeleo katika kata hiyo ikiwemo mradi wa ujenzi wa Zahanati Lyabusalu, ujenzi wa Choo cha shule ya msingi Lyabusalu B, ujenzi wa madarasa mawili shule ya msingi Lyabusalu A, ujenzi wa madarasa matatu katika shule ya msingi Bukamba pamoja na ujenzi wa nyumba ya walimu shule ya msingi Mwajiji.

Pia wamempongeza kwa usimamizi mzuri katika ujenzi wa darasa moja katika shule ya msingi Mwabagehu, ujenzi wa ofisi ya kijiji Mwabagehu, ujenzi wa Zahanati kijiji cha Mwashilugula, ujenzi wa shule mpya ya sekondari katika kijiji cha Mwasingu pamoja na ujenzi wa ofisi ya kata Lyabusalu ambapo fedha za miradi zinatoka serikali kuu na zingine katika mfumo wa jimbo.

Wakati huo huo madiwani wa viti maalum Halmashauri ya Wilaya ya Shinyanga wakiongozwa na mwenyekiti wao wamempongeza diwani wa kata ya Iselamagazi Mhe. Isaack Sengerema kwa usimamizi mzuri wa miradi ya maendeleo inayotekelezwa ili kutatua kero na changamoto za wananchi.

“Tunampongeza sana diwani wa kata ya Iselamagazi ipo miradi tumeitembelea tumeona hatua ni nzuri hasa ujenzi wa bweni la watoto wenye mahitaji maalum shule ya msingi Iselamagazi ambao tumeona mradi umefikia hatua ya upauaji lakini pia kuna ujenzi wa vyumba sita vya madarasa na matundu nane shule ya sekondari na tumeambiwa mradi huu umefikia hatua ya mwisho”.

“Pia kuna mradi wa uvutaji maji shule ya msingi Budushi tumeambiwa mradi huu umekamilika kwahiyo tunampongeza sana diwani na mbunge wa jimbo letu la Solwa lakini pia kuna mradi wa kituo cha Polisi Iselamagazi ambao tayari umekamilika pamoja na ujenzi wa ofisi ya kijiji cha Iselamagazi ambapo tumeambiwa boma limepauliwa kwahiyo tunampongeza tena mbunge kwa kupambania upatikanaji wa fedha za miradi pia tunampongeza diwani Isaack na Rais wetu Mama Samia kwa kutoa fedha za utekelezaji wa miradi ya maendeleo”.amesema Mhe. Zawadi

Madiwani wa viti maalum katika ziara yao wameendelea kuwakumbusha wanawake na wanachama wa CCM kuhakikisha wanakuwa kipaumbele katika hatua zote za uchaguzi wa serikali za mitaa unaotarajiwa kufanyika badae Mwaka huu 2024 pamoja na uchaguzi mkuu Mwaka 2025 ikiwemo zoezi la kujiandikisha kwenye daftari ya balozi pamoja na daftari ya mpiga kura.

Katibu wa umoja  wa wanawake UWT Wilaya ya Shinyanga vijijini Bi. Magdalena Dodoma  ameendelea kuwasisitiza wanawake wa UWT kujiamini na kuhakikisha wale wenye sifa wanachukua fomu kugombea nafasi mbalimbali za uongozi  katika vijiji na vitongoji wakati utakapofika .

Pia amesisitiza wanachama kujisajili kwenye mfumo wa kielekroniki ili kuendelea kuwa wanachama imara wa Chama cha Mapinduzi CCM.

Baadhi ya wanachama wa CCM na jumuiya zake wamewapongeza madiwani wa viti maalum kwa kufanya ziara hiyo ambapo wameahidi kuzingatia yale yote ambayo wamekumbushwa iliwemo kuchua fomu za kugombea nafasi mbalimbali za uongozi.

Pia wametumia nafasi hiyo kuiomba serikali kuwachukua hatua kali za kisheria watu wanaobainika kufanya vitendo vya ukatili ikiwemo upakaji na ulawiti kwa watoto.

Wameendelea kusema kuwa ni vema serikali kuendelea kuchukua hatua kali pia kwa wazazi wanaoshiriki katika ndoa za utotoni ambazo zinachangia kukatisha ndoto za watoto hasa wanafunzi kukosa haki yao ya elimu shuleni.

Katibu wa umoja  wa wanawake UWT Wilaya ya Shinyanga vijijini Bi. Magdalena Dodoma   akiwatambulisha madiwani baada ya kuwasili katika mkutano wao kata ya Lyamidati

.






Post a Comment

0 Comments