Ticker

6/recent/ticker-posts

MAKALA: DANIEL PATRICK KAPAYA ATOA AHADI KUU BAADA YA KUTEULIWA KUWA KATIBU WA SMAUJATA KANDA YA ZIWA: "NITAPAMBANA KWA UADILIFU, NITATEMBEA KILA MKOA KUPAMBANA NA UKATILI"

Na Mapuli Kitina Misalaba

 Tarehe 23 Agosti 2024 itabaki kuwa siku ya kukumbukwa kwa Daniel Patrick Kapaya, alipochukua rasmi majukumu ya kuwa Katibu wa Jumuiya ya Shujaa wa Maendeleo na Ustawi wa Jamii Tanzania (SMAUJATA) kwa Kanda ya Ziwa.

Baada ya kuteuliwa, Kapaya ameahidi kwa sauti kubwa kupambana na ukatili katika kanda hiyo, huku akisisitiza umuhimu wa ushirikiano wa karibu na viongozi wa serikali, mashirika yasiyo ya kiserikali, na wananchi kwa ujumla.

Shukrani kwa Uongozi wa Taifa: "Mwenyekiti Sospeter Bulugu na Viongozi Wengine Wameniamini"

Kapaya alitumia fursa ya siku hiyo kutoa shukrani zake za dhati kwa uongozi wa taifa wa SMAUJATA, akianza na Mwenyekiti wa Jumuiya hiyo, Sospeter Bulugu, ambaye alifanya uamuzi wa kumteua yeye kama Katibu wa Kanda ya Ziwa.

"Nitumie fursa hii kuushukuru uongozi wangu wa taifa, nikianza na Mwenyekiti wangu Sospeter Bulugu aliyeniteua kuwa Katibu wa SMAUJATA Kanda ya Ziwa, pamoja na waandamizi wake akiwemo Kamishna Hashim Omary na viongozi wengine waandamizi kwa kuniona nafaa kusimamia Kanda ya Ziwa," alisema Kapaya kwa furaha.

Aliendelea kwa kusema, "Nisema tu kwamba katika kuniteua huku hawajakosea nitapambana katika mikoa yangu sita na nitafanya kazi kwa uadilifu nitatembea kila mkoa kuhakikisha ukatili uliopo tunaweza kuumaliza, pia nitahakikisha viongozi wa mikoa yangu wanafanya kazi kwa haraka zaidi katika kuwafikia wahanga wanaopata ukatili wa kijinsia."

Katika hotuba yake, Kapaya alisisitiza kuwa SMAUJATA inafanya kazi kwa karibu sana na Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum, ambayo inaongozwa na Dkt. Dorothy Gwajima.

 Alisema, "Niishukuru Wizara ya Maendeleo ya Jamii ambayo tunafanya nayo kazi kwa pamoja, inayosimamiwa na Dkt. Dorothy Gwajima kwa ukaribu kabisa yupo bega kwa bega na SMAUJATA, na SMAUJATA inafanya kazi kwa moyo mmoja ikiona kabisa wizara hii inatupa ushirikiano."

Kapaya aliwahimiza maafisa ustawi wa jamii, maafisa maendeleo ya jamii, na Dawati la Jinsia kushirikiana nao kikamilifu huku akiendelea kuomba viongozi wa mikoa yao kuwa mstari wa mbele katika kushirikiana na SMAUJATA kwa lengo la kutokomeza ukatili.

"Niombe basi viongozi waliopo katika mikoa yetu waweze kusimama na sisi bega kwa bega kama Waziri Dorothy Gwajima anavyopambana na SMAUJATA,".alisema Kapaya

Vipaumbele vya Kapaya katika Kanda ya Ziwa: "Kupambana na Ukatili na Kutoa Haki kwa Makundi Maalum"

Kapaya aliweka wazi kuwa moja ya vipaumbele vyake kuu itakuwa ni kuhakikisha haki za msingi zinatolewa hasa kwa watoto, wanawake, vijana, na watu wenye ulemavu ambao ni makundi maalum katika maeneo yao.

Alizungumza kwa uchungu kuhusu suala linalotrendi kwenye mitandao ya kijamii la utekaji wa watoto, akisema, "Kwa kweli hatuna raha kama SMAUJATA, mimi kama kiongozi wa kanda nitaweza kulisimamia pamoja na viongozi walioko kwenye mikoa walifanyie kazi haraka kweli."

Kipaumbele kingine cha Kapaya ni kutembelea maeneo ya migodi katika Kanda ya Ziwa, ili kuhakikisha utekelezaji wa sera zinazozungumzia kuzuia ukatili wa kijinsia.

Alisema, "Kuna watoto wanaajiriwa katika umri mdogo, lakini vile vile tunaangalia na unyanyasaji wa kwenye migodi pengine kuna watu hawapati haki zao za msingi kama Katibu wa Kanda ya Ziwa, nitaweza kufanya hivyo na niwaombe tu viongozi wa mikoa nitakapoanza kufanya ziara zangu waweze kuniandalia sehemu zenye migodi tupite kwa ajili ya kuangalia utekelezaji wa sera zinazozungumzia kuzuia ukatili wa kijinsia."

Elimu ya Ukatili wa Kijinsia na Utengenezaji wa Timu ya Mashujaa: "Tuzidishe Ushirikiano ili Tupambane na Ukatili"

Kapaya pia alisisitiza umuhimu wa kutoa elimu ya ukatili wa kijinsia na kuhakikisha kuwa kila mkoa unajenga timu kubwa ya mashujaa wanaopinga ukatili.

Alisema, "Naiomba kila mkoa uhakikishe imetengeneza timu kubwa ya mashujaa waeleweke kwenye data bezi ya SMAUJATA lengo kubwa ni kupunguza uhalifu wa vitendo vya ukatili."

Kwa kumalizia, aliomba serikali iweze kutoa ushirikiano kwa viongozi wa SMAUJATA, hasa wanapokuwa wanatekeleza majukumu yao katika ngazi za chini. "Niwaombe sana maafisa ustawi wa jamii, maafisa maendeleo ya jamii, na Dawati la Jinsia mnapoona shujaa amekuja kiongozi wa SMAUJATA mmpe ushirikiano ili awe na moyo wa kufanya kazi," alihimiza.

Ahadi ya Kapaya kwa Kanda ya Ziwa: "Nipo Bega kwa Bega Kupambana na Ukatili"

Kapaya alihitimisha hotuba yake kwa kuahidi kutoa ushirikiano wakati wote kwa wananchi na viongozi wa SMAUJATA katika Kanda ya Ziwa. Alisema, "Ninaahidi kutoa ushirikiano wakati wote endapo kuna matatizo yoyote ya ukatili msisite kunijulisha, mimi nipo bega kwa bega na nitafanya kazi muda wowote na saa yoyote pindi mtakaponihitaji."

Aidha, alitoa shukrani maalum kwa Mkoa wa Shinyanga kwa ushirikiano mkubwa waliompa wakati alipokuwa Katibu wa SMAUJATA Mkoa wa Shinyanga alisema, "Kwa kweli tumefanya kazi vizuri na tumeweza kupambana na ukatili tukishirikiana na viongozi wangu wa SMAUJATA kwa kweli, ukatili Mkoa wa Shinyanga umeweza kupungua."

Kumbuka kuwa Bwana Daniel Patrick Kapaya aliteuliwa kuwa katibu wa SMAUJATA Mkoa wa Shinyanga Tarehe 24 Mwezi wa sita(6)  Mwaka  2023 na sasa ni katibu wa SMAUJATA kanda ya ziwa ambapo atasimamia mikoa sita ambayo ni  Shinyanga, Mwanza, Simiyu, Mara, Geita na Kagera.

Maombi kwa Wazazi: "Wachungeni Watoto, Tupunguze Vitendo vya Utekaji"

Kapaya alimaliza kwa kuwasihi wazazi kuchukua hatua madhubuti katika kuwalinda watoto wao. Alisema, "Nipande tu kuwaasa wazazi sasa wakae vizuri na watoto, wawe wanawachunguza na kuwalinda ili tupunguze vitendo vya utekaji pia watoto wapate elimu, lishe bora, na mafundisho ya kidini ili wakue wakiwa na hofu ya Mungu."

Kwa ujumla, Daniel Patrick Kapaya anaonekana kuwa na nia thabiti ya kuleta mabadiliko makubwa katika mapambano dhidi ya ukatili katika Kanda ya Ziwa, huku akihimiza ushirikiano wa kila mmoja katika kuhakikisha jamii inakuwa salama na yenye haki.

Jumuiya ya Shujaa wa Maendeleo na Ustawi wa Jamii Tanzania (SMAUJATA) ni jumuiya ya kupinga ukatili nchini inayotekeleza majukumu yake chini ya wizara ya maendeleo ya jamii, jinsia, wanawake na makundi maalum.

 

Post a Comment

0 Comments