Ticker

6/recent/ticker-posts

MTUHUMIWA WA KUMJERUHI MWANAMKE KWA KUMTOBOA MACHO AKAMATWA SHINYANGA

Na Mapuli Kitina Misalaba

Jeshi la Polisi Mkoa wa Shinyanga limefanikiwa kumkamata Paul Shija (19), mkazi wa kata ya Ndala, Manispaa ya Shinyanga, kwa tuhuma za kumjeruhi Ester Matalanga (25), ambaye ni mkazi wa eneo hilo.

Tukio hilo limemhusisha Shija, ambaye alikuwa mume wa zamani wa Esther Matalanga.

Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na Kamanda wa Polisi Mkoa wa Shinyanga, SACP Janeth Magomi, tukio hilo lilitokea mnamo tarehe 13 Agosti 2024 ambapo Ester Matalanga alijeruhiwa  kwa kutobolewa macho yake yote mawili na Paul Shija, ambaye alikuwa mume wake wa zamani.

Jeshi la Polisi lilichukua hatua za haraka kufika eneo la tukio, ambapo walimchukua Matalanga na kumpeleka katika Hospitali ya Kolandoto, iliyopo Manispaa ya Shinyanga, kwa ajili ya matibabu ya haraka.

Kamanda Magomi amesema kuwa upelelezi wa tukio hilo bado unaendelea, na mara baada ya kukamilika, sheria itachukua mkondo wake ili kuhakikisha haki inatendeka.

Aidha, Kamanda Magomi amewataka wananchi waendelee kushirikiana na jeshi la Polisi kwa kutoa taarifa zinazohusu wahalifu na uhalifu katika maeneo yao.

 Ameweka wazi kuwa taarifa za kiintelijensia kutoka kwa raia wema ndizo zilizosababisha mafanikio ya kukamatwa kwa mtuhumiwa huyo, ambaye alikutwa nyumbani kwake kutokana na taarifa za siri kutoka kwa wasamaria wema.

Jeshi la Polisi linaendelea kuhimiza raia kuachana na tabia ya kujichukulia sheria mkononi, likisisitiza kuwa hatua kali za kisheria zitachukuliwa kwa yeyote atakayehusika na vitendo vya aina hiyo.

Tukio hilo limeibua hisia kali miongoni mwa wakazi wa Shinyanga, wengi wakilaani kitendo hicho na kuitaka jamii kuungana kupinga ukatili wa kijinsia.

Tunaendelea kufuatilia kwa karibu upelelezi wa tukio hili na hatua zaidi kutoka kwa mamlaka husika, huku tukilenga kutoa taarifa za kina kwa wananchi kupitia MISALABA MEDIA.

TAZAMA VIDEO

Post a Comment

0 Comments