Ticker

6/recent/ticker-posts

WANAFUNZI ZAIDI YA 45,000 MKOANI SHINYANGA KUWAANZA MTIHANI WA KUMALIZA DARASA LA SABA, MKUU WA MKOA ATOA ONYO JUU YA UDANGANYIFU

Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga Mhe. Anamringi Macha akizungumza na waandishi wa habari ofisi kwake.

Na Mapuli Kitina Misalaba

Jumla ya wanafunzi 45,693 mkoani Shinyanga wanatarajia kuanza mtihani wa kuhitimu elimu ya msingi kesho, huku Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga, Anamringi Macha, akionya vikali dhidi ya udanganyifu katika mitihani hiyo.

Akizungumza na waandishi wa habari leo Septemba 10, 2024, Mkuu huyo wa mkoa ameeleza kuwa mtihani wa darasa la saba utaanza kesho na kumalizika kesho kutwa, ukihusisha wavulana 19,528 na wasichana 26,165.

Ameongeza kuwa serikali haitasita kuchukua hatua kali kwa shule, hususan za binafsi, zitakazobainika kujihusisha na udanganyifu wa mitihani.

"Shule za binafsi mara nyingi zinakuwa na ushindani mkali wa kutaka wanafunzi wafaulu ili kupata sifa, lakini sitaruhusu udanganyifu wa aina yoyote shule itakayokutwa inafanya udanganyifu itafungiwa mara moja," amesema Macha.

Ameonya pia shule za serikali, walimu, na wazazi kutojihusisha na udanganyifu ambapo amesisitiza kuwa ni muhimu kwa wanafunzi kuonyesha kile walichojifunza ndani ya miaka saba badala ya kusaidiwa kwa njia zisizo halali.

"Walimu na wazazi wasiwadanganye watoto, na wazazi pia wasiwashawishi watoto kufanya vibaya kwa nia ya kuwaoza au kuwafanya wachungaji wa mifugo," amesisitiza.

Aidha, Mkuu huyo wa mkoa ameweka wazi kuwa maandalizi ya mitihani yamekamilika, na walimu 3,339 wamepangwa kusimamia mitihani hiyo.

Baadhi ya wanafunzi wa darasa la saba, akiwemo Mariamu Amosi kutoka shule ya msingi Mwenge, wamesema wako tayari kwa mitihani hiyo na wana matumaini ya kupata matokeo mazuri.

 

Post a Comment

0 Comments