Ticker

6/recent/ticker-posts

WAZIRI BASHE AAINISHA MIKAKATI YA KUIMARISHA SEKTA YA KILIMO, MIFUMO YA TEHAMA KULETA MAPINDUZI YA KILIMO SHINYANGA


Na Mapuli Kitina Misalaba

Waziri wa Kilimo Mhe. Hussein Mohammed Bashe, ameweka wazi mipango na hatua zinazochukuliwa na wizara hiyo ili kuboresha sekta ya kilimo, hususan katika mkoa wa Shinyanga, ambao una mchango mkubwa kwenye uzalishaji wa mazao muhimu nchini.

Waziri Bashe ameyasema hayo katika ziara yake Mkoani Shinyanga, wakati akizungumza kwenye kikao ambacho kimehudhuriwa na viongozi mbalimbali wakiwemo wakuu wa Wilaya, wakurugenzi wa Halmashauri, maafisa kilimo pamoja na wafanyabiashara wa mazao Mkoani Shinyanga.

Sekta ya kilimo ni nguzo kuu ya uchumi wa Tanzania, ambapo mwaka 2022 ilichangia asilimia 26.2 ya Pato Ghafi la Taifa (GDP) ambapo kilimo kinatoa asilimia 65 ya malighafi za viwanda na kutoa ajira kwa asilimia 65.6 ya Watanzania (NBS, 2020), huku kikiwa chanzo cha asilimia 30 ya fedha za kigeni zinazopatikana nchini.

Waziri Bashe ameeleza kuwa serikali imejipanga kusimamia kilimo-biashara kwa kushirikiana na sekta binafsi, ambayo ni mdau muhimu katika kukuza sekta hii.

Amesema mchango wa teknolojia na utafiti wa kisasa unaendelea kupewa kipaumbele, sambamba na kuhakikisha kuwa sera na sheria zinalinda ardhi ya kilimo na kuimarisha mifumo ya masoko.

Mkoa wa Shinyanga umeendelea kuwa na mchango mkubwa katika uzalishaji wa mazao mbalimbali, lakini bado kuna changamoto za kuongeza tija kwa mujibu wa Mkurugenzi wa maendeleo ya mazao Wizara ya Kilimo Bwana Nyasebwa Chimagu amesema Mkoa wa Shinyanga unashika nafasi ya 15 kati ya mikoa 26 kwa uzalishaji wa nafaka, ambapo unalimwa hekta 341,042 na kuzalisha tani 465,180.

Kwa mazao yasiyo ya nafaka, Shinyanga inashika nafasi ya 18, ikilima hekta 211,012 na kuzalisha tani 239,021 hata hivyo, tija ya mazao kama mahindi na mchele inabaki chini ya wastani wa kitaifa.

Mahindi huzalishwa kwa tani 1.3 kwa hekta, na mchele kwa tani 1.4, hali inayodhihirisha umuhimu wa kuzingatia matumizi ya kanuni bora za kilimo ili kuongeza uzalishaji na kuyafikia masoko ya ndani na nje kwa ufanisi zaidi.

Mkurugenzi wa maendeleo ya mazao Wizara ya Kilimo Bwana Nyasebwa Chimagu amebainisha kuwa katika mwaka wa fedha wa 2024/2025, wizara hiyo imepanga kuongeza nguvu katika maeneo yafuatayo:

Kuongeza tija na uzalishaji – Serikali itaendelea kuhamasisha matumizi ya teknolojia bora na kuongeza upatikanaji wa pembejeo kwa wakulima.

Kuongeza ajira kwa vijana na wanawake – Serikali inalenga kuongeza ajira zenye staha kupitia kilimo, kwa kuhamasisha ushiriki wa vijana na wanawake.

Kuimarisha usalama wa chakula na lishe – Lengo ni kuhakikisha uzalishaji wa mazao unakidhi mahitaji ya chakula nchini.

Kuimarisha masoko na mitaji – Upatikanaji wa masoko na mitaji utaendelea kupewa kipaumbele, ili kuimarisha usafirishaji wa mazao nje ya nchi na kuongeza mapato ya wakulima.

Kuimarisha ushirika – Serikali itaendelea kuhamasisha maendeleo ya vyama vya ushirika katika kilimo ili kuongeza ufanisi.

Matumizi ya mifumo ya TEHAMA – Mfumo wa kidigitali utaimarishwa ili kurahisisha huduma kwa wakulima na kukuza maendeleo ya sekta hii.

Kwa upande wake mkuu wa Mkoa wa Shinyanga Mhe. Anamringi Macha amesema serikali itaendelea kushirikiana na wakulima pamoja na wadau wa mazao ili kuleta matokeo chanya kwenye sekta ya Kilimo.

Mwenyekiti wa wafanyabiashara wa mazao Mkoa wa Shinyanga Bwana Hassan Mboje amepongeza kwa ushirikiano wa serikali huku akiiomba serikali kutatua haraka changamoto zilizopo.

Naye mkurugenzi mkuu wa Bodi ya Pamba, Marco Mtunga amesema zipo fursa mbalimbali katika zao hilo hivyo amewahimiza wakulima kuchangamkia fursa zinazojitokeza.

Waziri wa Kilimo Mhe. Hussein Mohammed Bashe, akizungumza.


Post a Comment

0 Comments