Ticker

6/recent/ticker-posts

DIWANI WA KATA YA NGOKOLO VICTOR MKWIZU AJIANDIKISHA KATIKA DAFTARI LA WAKAZI ATOA TOFAUTI KATI YA UCHAGUZI WA MTAA NA UCHAGUZI MKUU

Na Mapuli Kitina Misalaba

Katika jitihada za kuhakikisha wakazi wa Shinyanga wanashiriki kikamilifu kwenye uchaguzi wa serikali za mitaa, zoezi la uandikishaji wakazi limeanza rasmi tarehe 11 Oktoba na litarajiwa kumalizika tarehe 20 Oktoba.

Uchaguzi wa kumchagua mwenyekiti wa mtaa utafanyika tarehe 27 Novemba, mwaka huu, huku wakazi wa kata ya Ngokolo wakihimizwa kujitokeza kwa wingi katika zoezi hilo muhimu.

Akizungumza baada ya kujiandikisha katika kituo cha Madaktari Bingwa kilichopo mtaa wa Majengo Mapya, Diwani wa kata ya Ngokolo, Mhe. Victor Yessaya  Mkwizu, ameonyesha hamasa kubwa kwa wananchi wa kata yake kujiandikisha.

“Leo nimepata fursa ya kuja kujiandikisha kwa ajili ya kumchagua mwenyekiti wangu wa serikali ya mtaa, Tunajiandikisha kwenye daftari la makazi kwa ajili ya kumchagua mwenyekiti wetu wa serikali ya mtaa, kwahiyo nawaomba wakazi wote wajitokeze ili waweze kutimiza haki yao ya kidemokrasia.”amesema Mkwizu

Kata ya Ngokolo ina jumla ya mitaa saba, na kwa mujibu wa Diwani Victor Mkwizu, ni muhimu wakazi wote wa mitaa hiyo wajitokeze ili kuhakikisha kuwa uchaguzi unafanyika kwa mafanikio na uwazi.

“Niwaombe wakazi wote wa kata ya Ngokolo, kwenye mitaa yote saba, mjitokeze kwa ajili ya kwenda kujiandikisha kwenye daftari la wakazi ili muweze kumchagua mwenyekiti wa mtaa wenu,” amesema Mkwizu.

Diwani Mkwizu pia amefafanua kwamba kumekuwa na mkanganyiko kwa baadhi ya wakazi kuhusu mchakato huu wa uandikishaji, ambapo wengine wanadhani ni uandikishaji kwa ajili ya uchaguzi mkuu wa mwaka 2025.

Amefafanua tofauti kati ya zoezi hilo la sasa na uandikishaji wa kudumu wa wapiga kura wa Tume ya Uchaguzi.

“Hili zoezi tunalofanya sasa ni tofauti na uandikishaji wa wapiga kura wa mwaka 2025. Hili ni kwa ajili ya uchaguzi wa serikali za mitaa kwa ajili ya kuchagua viongozi wa mitaa yetu. Kwa hiyo, nawasihi wananchi wote wajitokeze kwa wingi kushiriki zoezi hili muhimu kwa maendeleo ya mtaa na kata yetu kwa ujumla,” amesema Diwani  Mkwizu.

Zoezi hilo la uandikishaji linaendelea kwa siku kumi, likihitimishwa tarehe 20 Oktoba, likiwa na lengo la kuwezesha uchaguzi huru na wa haki, ambapo viongozi wa mitaa watakaochaguliwa watakuwa na jukumu kubwa la kuleta maendeleo katika maeneo yao.

Wakazi wa Shinyanga, hususan kutoka kata ya Ngokolo, wanatarajiwa kujitokeza kwa wingi ili kuhakikisha wanaweka viongozi wanaowaamini na watakaosimamia vyema maendeleo ya jamii zao.

Diwani wa kata ya Ngokolo, Mhe. Victor Yessaya  Mkwizu, akijiandikisha kwenye daftari la wakazi.


 

Post a Comment

0 Comments