Ticker

6/recent/ticker-posts

KATIBU WA ACT WAZALENDO JIMBO LA SHINYANGA MJINI JUSTER DENIS AHAMASISHA UANDIKISHAJI WAKAZI UCHAGUZI WA SERIKALI ZA MITAA

Na Mapuli Kitina Misalaba

Katibu wa chama cha ACT Wazalendo jimbo la Shinyanga mjini, ambaye pia ni mjumbe wa Halmashauri Kuu Taifa na Naibu Waziri Kivuli wa Jinsia, Maendeleo ya Wanawake, Watoto na Makundi Maalum, Bi. Juster Denis amejitokeza kujiandikisha kwenye daftari la wakazi katika kituo cha shule ya msingi Ndembezi.

Tukio hilo linatokea kuelekea uchaguzi wa Serikali za Mitaa ambapo Bi. Juster amesisitiza umuhimu wa wananchi kujitokeza kwa wingi ili kuchagua viongozi bora.

Bi. Juster ameeleza kuwa moja ya sababu kubwa ya kujitokeza kwake ni kuhamasisha wananchi, hususan vijana, ili waweze kushiriki kikamilifu kwenye mchakato wa uchaguzi.

"Nimekuja hapa kujiandikisha lakini pia kuwahamasisha wananchi kujitokeza kwa wingi ili tupate viongozi bora. Ni muhimu vijana wajitokeze, wasiwe wa kusema tu na hawajajiandikisha kwenye daftari la wapiga kura," amesema Juster.

Bi. Juster ametumia fursa hiyo kuzungumzia changamoto zinazolikabili eneo la Ndembezi, akitolea mfano wa miundombinu duni, ikiwemo ukosefu wa barabara licha ya kuwa eneo hilo ni sehemu ya Manispaa.

Amesisitiza kuwa upatikanaji wa kiongozi bora ni njia ya kuleta mabadiliko ya kweli kwa wananchi wa eneo hilo.

 "Hii Ndembezi ni eneo la Manispaa lakini tangu liingizwe kwenye ramani hiyo halina barabara, ni wakati sasa wa kuchagua viongozi wanaoweza kubadilisha hali hii tunataka mabadiliko, tuchague ACT Wazalendo ili tuweze kuvuka kutoka tulipo kwenda sehemu nyingine," amesema Juster

Katika mazungumzo yake, Bi. Juster amekosoa tabia ya wanasiasa kutumia ahadi za miradi hewa kama vile ujenzi wa zahanati ambazo hazikamiliki kwa miaka mingi kama njia ya kupata kura.

Amesema chama chake cha ACT Wazalendo kinajikita katika kuleta mabadiliko ya kweli kwa wananchi na siyo kuahidi miradi ambayo haitekelezeki.

 "Tunamsingi wa zahanati ambao umekuwa ukitumika kuombea kura kwa miaka mingi, sisi ACT Wazalendo hatutaki hayo tunataka mabadiliko halisi kwa wananchi," amesema Juster.

Misalaba Media  imezungumza na baadhi ya wanawake wakazi wa mtaa wa Ndembezi ambao tayari wamejiandikisha kwenye daftari la wakazi na kwamba wamehamasisha wanawake wenzao kujitokeza kwa wingi na kushiriki kwenye zoezi la uchaguzi.

Wamesema ni muhimu kwa wanawake kujitokeza ili kuhakikisha wanapata viongozi wa mtaa wanaofaa ambao watazingatia maslahi ya wananchi wote.

Uchaguzi wa serikali za mitaa ukikaribia, hamasa inaonekana kuongezeka kwa wananchi wa Shinyanga mjini, huku viongozi wa vyama vya siasa wakihimiza umuhimu wa uandikishaji wa wakazi kama hatua ya awali ya kushiriki kikamilifu katika uchaguzi.

Katibu wa chama cha ACT Wazalendo jimbo la Shinyanga mjini, ambaye pia ni mjumbe wa Halmashauri Kuu Taifa na Naibu Waziri Kivuli wa Jinsia, Maendeleo ya Wanawake, Watoto na Makundi Maalum, Bi. Juster Denis akijiandikisha kwenye daftari la wakazi.


 

Post a Comment

0 Comments