Ticker

6/recent/ticker-posts

MBUNGE KATAMBI ATOA MAOMBI YA MIRADI YA MAENDELEO SHINYANGA, KATIBU MKUU WA CCM ATOA MAELEKEZO YA KUJENGA BARABARA, KITUO CHA AFYA IBADAKULI

 Na Mapuli Kitina Misalaba

Katibu Mkuu wa Chama cha Mapinduzi (CCM), Balozi Dkt. Emmanuel Nchimbi, amechukua hatua kubwa katika kutatua changamoto za wananchi wa Kata ya Ibadakuli kwa kutoa maelekezo ya ujenzi wa Kituo cha Afya katika eneo hilo.

Akiwa mbele ya umati wa wananchi, viongozi wa chama na Serikali, Dkt. Nchimbi ametoa agizo rasmi kwa Waziri wa TAMISEMI, Mohammed Mchengerwa, kuhakikisha ujenzi wa kituo hicho unaanza mara moja.

Balozi Dkt. Nchimbi ametoa wito kwa Serikali kuchukua hatua za haraka ili kuhakikisha wananchi wa Ibadakuli wanapata huduma bora za afya.

“Nichukue nafasi hii kumuelekeza Waziri wa TAMISEMI, Mohammed Mchengerwa, popote alipo, hili ni agizo la Chama cha Mapinduzi (CCM), kuhakikisha Kituo cha Afya Ibadakuli kinaanza kujengwa mara moja. Natambua yeye ni miongoni mwa Mawaziri wasikivu na wachapakazi," amesema Dkt. Nchimbi,

Agizo hili linakuja kufuatia maombi yaliyotolewa na Mbunge wa Jimbo la Shinyanga Mjini, Patrobas Katambi, ambaye ni Naibu Waziri katika Ofisi ya Waziri Mkuu (Kazi, Vijana, Ajira na Watu Wenye Ulemavu) Mhe. Paschal Patrobas Katambi.

 Katika mkutano huo wa hadhara, Katambi ameelezea uhitaji mkubwa wa huduma za afya kwa wananchi wa Kata ya Ibadakuli, pamoja na umuhimu wa kukarabati Hospitali ya Manispaa na barabara ambazo zimeathiriwa vibaya na mvua za msimu.

Amesema kuwa wananchi wa Ibadakuli wamekuwa na changamoto ya muda mrefu ya ukosefu wa huduma za afya za karibu, hivyo ameiomba Serikali kuwekeza katika ujenzi wa kituo hicho.

Aliongeza kuwa mbali na afya, eneo hilo pia linahitaji ukarabati wa Hospitali ya Manispaa ya Shinyanga pamoja na barabara zilizoathiriwa na mvua.

Mbunge Katambi pia ametumia fursa hiyo kumpongeza Rais Samia Suluhu Hassan kwa mchango wake mkubwa katika maendeleo ya Jimbo la Shinyanga mjini, akibainisha miradi mingi inayotekelezwa, ikiwa ni pamoja na ujenzi wa uwanja wa ndege, miundombinu ya barabara, na Hospitali.

“Rais Samia Suluhu Hassan amewekeza sana katika jimbo letu, na tumeona maendeleo makubwa, ikiwemo ujenzi wa uwanja wa ndege Ibadakuli, barabara, na madaraja. Hata hivyo, tunahitaji zaidi katika sekta ya afya na miundombinu,” naomba mfikishe salamu za shukrani kwa Rais kutokana na miradi hiyo ya maendeleo”.

“Tunatoa shukrani za dhati kwa Rais wetu kwa fedha nyingi alizotoa kwa ajili ya kuboresha huduma za afya, ikiwemo ujenzi wa vituo vipya vya afya, Hospitali, na zahanati saba za kisasa,” amesema Katambi.

 Mhe. Katambi amewataka wananchi kuendelea kumuunga mkono Rais Samia kwa kazi zake nzuri za kuwaletea maendeleo.

Katika hatua nyingine, Dkt. Nchimbi ameagiza ushirikiano baina ya Waziri wa TAMISEMI na Waziri wa Ulinzi, Dkt. Stergomena Tax, kuhakikisha mgogoro baina ya Jeshi na wananchi wa Shinyanga unatatuliwa kwa njia ya amani.

 Ameitaka TARURA kuharakisha ukarabati wa barabara zote zilizoharibika, ili wananchi waendelee kunufaika na miundombinu bora.

Akihitimisha hotuba yake, Katibu Mkuu Nchimbi ametoa wito kwa wananchi wa Shinyanga kujiandikisha kwenye daftari la wakazi, ikiwa ni sehemu ya maandalizi ya uchaguzi wa Serikali za Mitaa unaotarajiwa kufanyika Novemba 27.

Amesisitiza kuwa zoezi la kujiandikisha linaendelea hadi Oktoba 20 na akatoa mfano wa Rais Samia Suluhu Hassan, ambaye tayari amejiandikisha.

Katibu wa NEC, Itikadi, Uenezi, na Mafunzo, Ndugu Amos Makalla, ameungana na viongozi wengine kumpongeza Mbunge Mhe. Katambi kwa juhudi zake za kuwaletea wananchi maendeleo.

Amewaambia wananchi kuwa Shinyanga ya sasa si ile ya zamani, kwani imepiga hatua kubwa kimaendeleo kutokana na uwekezaji wa Serikali ya awamu ya sita.

MISALABA MEDIA imezungumza na baadhi ya wakazi wa Shinyanga Mjini ambao wametoa pongezi kwa Mbunge wao, Mhe. Patrobas Katambi, kwa juhudi zake za kufikisha changamoto zao kwa viongozi wa kitaifa.

Wakazi hao wamesema wanathamini kazi nzuri anayofanya Mbunge wao na wana imani kuwa Serikali itashughulikia haraka changamoto alizozibainisha, hususan uhitaji wa Kituo cha Afya katika Kata ya Ibadakuli.

Aidha, wakazi hao wameeleza kuwa ujenzi wa barabara kwa kiwango cha lami ni kipaumbele kwao, hasa barabara ya kutoka Ndala kwenda Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Shinyanga, Mwawaza ambapo wamesisitiza kuwa barabara hiyo ni muhimu kwa usafiri wa wagonjwa na pia itaongeza ufanisi wa huduma za afya katika Hospitali hiyo.

Wananchi hao wamesema wanatumaini kuwa hatua hizo zitachukuliwa kwa haraka ili kuboresha huduma za jamii na kuwezesha wananchi kupata maendeleo yanayoendana na kasi ya Serikali ya Awamu ya Sita.

Ziara ya Dkt. Nchimbi katika mikoa ya Simiyu na Shinyanga imetamatika kwa mafanikio makubwa, huku lengo kuu likiwa ni kukagua kukagua uhai wa chama, utekelezaji wa Ilani ya CCM na kusikiliza kero za wananchi katika maeneo mbalimbali.

Katibu Mkuu wa CCM Balozi Dk.Emmanuel Nchimbi (kushoto) akiwa na Mbunge wa Jimbo la Shinyanga Mjini Patrobasi Katambi ambaye pia ni Naibu Waziri Ofisi ya Waziri Mkuu,kazi,vijana,ajira na watu wenye ulemavu.

TAZAMA VIDEO

 

Post a Comment

0 Comments