Ticker

6/recent/ticker-posts

MBUNGE CHEREHANI AOMBA KAHAMA KUWA MKOA WA KI - TANESCO KUTATUA CHANGAMOTO ZA UMEME


Na Mapuli Kitina Misalaba

Mbunge wa Jimbo la Ushetu, Mhe. Emmanuel Cherehani, ametoa ombi la kuboreshwa kwa miundombinu ya barabara na huduma za umeme katika Wilaya ya Kahama wakati wa mkutano wa hadhara uliofanyika Oktoba 10, 2024 Manispaa ya Kahama.

 Akizungumza mbele ya Katibu Mkuu wa Chama cha Mapinduzi (CCM), Balozi Dkt. Emmanuel Nchimbi, pamoja na wananchi wa Kahama, Mhe. Cherehani amegusia mafanikio ya utekelezaji wa miradi lakini pia amesisitiza umuhimu wa marekebisho kadhaa katika huduma zinazotolewa na taasisi za umma.

Mhe. Cherehani amebainisha kuwa moja ya changamoto kubwa wanayokumbana nayo ni upungufu wa usimamizi wa barabara katika Halmashauri ya Ushetu.

 “Halmashauri ya Ushetu ilikuwa na Meneja wa TARURA aliyekuwa anasimamia barabara zote, lakini aliondolewa na sasa tunategemea meneja mmoja aliyepo Kahama eneo la Kahama ni kubwa sana, na hili linatuathiri  tunaomba turudishiwe meneja wetu ili kuhakikisha barabara zinakaguliwa ipasavyo na ziko katika hali nzuri,” amesema Chelehan.

Mhe. Cherehani pia amezungumzia changamoto ya kuwa na mkandarasi mmoja anayesimamia miradi ya ujenzi wa barabara katika majimbo yote matatu ya Wilaya ya Kahama - Ushetu, Msalala, na Kahama Mjini.

"Wilaya ya Kahama ni kubwa sana, lakini tunapewa mkandarasi mmoja tu kwa majimbo yote hili linaathiri kasi ya utekelezaji wa miradi, na wakati mwingine mkandarasi anakosolewa kwa kutokukamilisha kazi kwa wakati, ilhali ukubwa wa eneo ni changamoto kubwa kwake,” ameeleza Cherehani.

Ameendelea kuomba kuwa kila jimbo lipatiwe mkandarasi wake wa ujenzi ili kuhakikisha miradi inatekelezwa kwa ufanisi zaidi na kwamba ombi hili linaonekana kuwa la msingi, ikizingatiwa kuwa wilaya hiyo ina jiografia kubwa na miradi mingi inahusisha maeneo ya mbali.

Kahama Iwe Mkoa wa Ki-Tanesco

Katika hatua nyingine, Mhe. Chelehan amezungumza kuhusu tatizo sugu la kukatika kwa umeme mara kwa mara katika Wilaya ya Kahama ambapo ameomba Kahama ipandishwe hadhi kuwa Mkoa wa Ki-Tanesco ili kuhakikisha huduma za umeme zinaboreshwa.

 "Umeme unakatikakatika sana, hali hii inawaathiri sana wafanyabiashara na wananchi kwa ujumla wafanyabiashara wanapata hasara, na bei ya jenereta imepanda sana tunaomba Mkoa wa Ki-Tanesco ili na sisi Ushetu na Msalala tuweze kupata umeme wa uhakika,” amesema Cherehani.

Cherehani ameeleza kuwa kutokana na shughuli nyingi za kiuchumi katika wilaya hiyo, hasa za uchimbaji madini, kuna umuhimu mkubwa wa kuwa na usimamizi wa umeme wa karibu ili kuhakikisha huduma zinapatikana kwa uhakika na endelevu.

Katibu Mkuu CCM Apiga Simu kwa Waziri Biteko

Katibu Mkuu wa CCM, Balozi Dkt. Emmanuel Nchimbi, amelazimika kumpigia simu Naibu Waziri Mkuu na Waziri wa Nishati, Dkt. Dotto Biteko, kwa lengo la kupata muafaka kuhusu ombi hilo la kuongeza Mkoa wa Ki-Tanesco Kahama.

Katika mazungumzo ya simu, Mhe. Biteko amekiri kuwa Wabunge wa Kahama wamewasilisha maombi hayo mara kadhaa, na serikali tayari imelifanyia kazi suala hilo ambapo amesema kuwa utekelezaji wa mpango huo utaanza katika mwaka wa fedha 2024/2025.

"Tulipokea maombi kutoka kwa wabunge wa Kahama, na tumefanya uchambuzi wa kina kwenye maeneo yatakayopatiwa Mkoa wa Ki-Tanesco, Kahama itakuwa miongoni mwa maeneo yatakayopata huduma hii kutokana na umuhimu wake wa kiuchumi, hasa kutokana na migodi ya madini iliyopo katika eneo hilo," ameeleza Mhe. Biteko.

Mkutano huo umehudhuriwa na mamia ya wananchi wa Wilaya ya Kahama, ambapo Mhe. Chelehan ametumia nafasi hiyo kuelezea juhudi zake katika kutekeleza Ilani ya Uchaguzi ya CCM.

Amejivunia kuwa tangu awe mbunge, amefanya mikutano 274 ya hadhara, na kwa kushirikiana na viongozi wa kata, matawi, wilaya, na mkoa, amefanikiwa kutatua kero nyingi za wananchi.

Amewapongeza viongozi wa serikali, akiwemo Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga na Mkuu wa Wilaya ya Kahama, kwa ushirikiano mkubwa wanaouonesha katika kuleta maendeleo Ushetu.

Baada ya mkutano huo wa hadhara, Misalaba Media imezungumza na baadhi ya wakazi wa Wilaya ya Kahama, wakiwemo wananchi wa Jimbo la Ushetu, ambao wamempongeza Mbunge wao, Mhe. Emmanuel Cherehani, kwa juhudi zake za kusimamia maendeleo ya jimbo hilo.

Wakazi hao wameeleza kuwa changamoto alizozitaja mbunge zinaathiri kwa kiasi kikubwa shughuli zao za kiuchumi, huku wakiiomba serikali kuharakisha utatuzi wa matatizo hayo.

Wameeleza matumaini yao kwamba ombi la kuongeza Mkoa wa Ki-Tanesco litafanikishwa, wakiamini kuwa litasaidia kupunguza matatizo ya umeme ambayo yamekuwa yakiathiri biashara na maendeleo ya kijamii katika wilaya hiyo.

Kwa ujumla, wananchi wa Ushetu wamepongeza jitihada za Mhe. Chelehan, huku wakiendelea kuiomba serikali kushughulikia changamoto zilizopo kwa haraka ili kuboresha maisha yao na kuimarisha uchumi wa wilaya, mkoa, na taifa kwa ujumla.

Mkutano huu umetoa picha ya juhudi kubwa zinazofanywa na Mbunge wa Ushetu kuhakikisha kuwa wananchi wake wanapata huduma bora na miundombinu iliyoboreshwa pia umetoa matumaini kwamba ombi la Kahama kuwa Mkoa wa Ki-Tanesco litafanikishwa na serikali ndani ya muda mfupi.

 

Mbunge wa jimbo la Ushetu Mhe. Emmanuel Chelehan akielezea changamoto za wananchi katika mkutano wa hadhara Wilaya ya Kahama.


 

Post a Comment

0 Comments