Ticker

6/recent/ticker-posts

MR. BLACK AKABIDHI MSAADA WA VIFAA VYENYE THAMANI YA MILIONI 3.2 KWA SHULE NA VIKUNDI MANISPAA YA SHINYANGA

Na Mapuli Kitina Misalaba

Mkurugenzi wa THE BSL INVESTMENT COMPANY LIMITED na THE TRUE LIFE FOUNDATION, Peter Frank maarufu kama Mr. Black, leo amekabidhi msaada wa vifaa mbalimbali vyenye thamani ya shilingi milioni tatu na laki mbili (Tsh 3,200,000) kwa shule na vikundi vilivyopo Manispaa ya Shinyanga.

Hafla ya makabidhiano hayo imefanyika mjini Shinyanga, huku ikihudhuriwa na viongozi wa elimu, walimu, na wanajamii wa Shinyanga.

Msaada huo umejumuisha mabati, mifuko ya Saruji, kompyuta, vifaa vya michezo, pamoja na viti kwa ajili ya vikundi vya kijamii ambapo Shule zilizopokea msaada ni pamoja na Shule za Msingi Ushirika, Uhuru, Bugoyi B, Mapinduzi A, na Town vilevile, Shule za Msingi Mwenge na Kambarage, pamoja na timu ya vijana ya Kapina FC, wamepokea jezi za michezo.

Pia, ametoa viti 20 kwa vikundi vya Wakatoliki na Wazazi vilivyopo kata ya Kizumbi kama sehemu ya kuimarisha uchumi wa vikundi hivyo kwa kupitia kukodisha viti hivyo. "Nimewakabidhi viti ambavyo walivihitaji kwa ajili ya kukodisha ili wainuke kiuchumi,".

“Leo Shinyanga tunatoa zawadi ya shukrani kwenu kwa sababu mmekuwa mkitubeba katika shughuli zenu, mmekuwa mkitubeba katika makanisa yenu, na mmekuwa mkitubeba katika vikundi vyenu ama ofisi zenu mbalimbali leo tumekabidhi vifaa vyenye thamani ya milioni tatu na laki mbili kama shukrani yetu ya dhati kwa ofisi ambazo tumekuwa tukishirikiana nazo, na huu ni mwanzo tu, tutakuja tena na awamu ya pili."amesema Mr. Black

Mr. Black ameeleza kuwa msaada huo ni sehemu ya sadaka na shukrani kwa jamii ya Shinyanga, akisisitiza kuwa yeye ni mdau namba moja wa maendeleo katika sekta za elimu, jamii, na uchumi nchini Tanzania.

"Nafanya haya yote kwa sababu ni sadaka iliyotukufu kutoka ndani ya moyo wangu na ni shukrani kwa watu wanaonisaidia katika shughuli zangu, Manufaa ya kwanza kuyaona mimi ni kuona nchi yangu inapata maendeleo na amani."amesema Mr. Black

"Rai yangu kwenu, tafsiri za Shinyanga ni nyingi, lakini viongozi ninaowatambua ni wachache wa kwanza ni Mhe. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania wa pili ni Mbunge wangu, Paschal Patrobas Katambi, na wa tatu ni Diwani wa Kata ya Kizumbi, Reuben Kitinya wengine waliopo katika nafasi zao pia nawathamini, lakini naomba tafsiri potovu zisiwepo huu msaada ni wa upendo, si wa kisiasa, na muda wa Mungu utakapofika, jina langu litakamilika."amesema Mr. Black

Mr. Black ameeleza historia yake yenye kutoa machozi na jinsi alivyolelewa ndani ya chama cha CCM baada ya wazazi wake kufariki akiwa mtoto mdogo ambapo amesema kuwa msaada anaoutoa unamtoa faraja na matumaini kwa jamii ambayo imekuwa ikimsaidia, huku akiahidi kuendelea kuwekeza katika maendeleo ya jamii.

Mgeni rasmi katika hafla hiyo, mwakilishi wa Mkuu wa Wilaya ya Shinyanga na Afisa Elimu Sekondari wa Manispaa ya Shinyanga, Lucas Mzungu ametoa pongezi kwa Mr. Black na kampuni ya THE BSL INVESTMENT COMPANY kwa juhudi za kurudisha fadhila kwa jamii.

"Naishukuru kampuni ya THE BSL kupitia mkurugenzi wake Mr. Black kwa hiki wanachokifanya cha kurudisha fadhila kwa jamii iliyowalea ni tukio la kufurahisha na lenye baraka. Mungu awabariki," amesema Mzungu.

Aidha Mzungu amewahimiza wale waliopokea msaada huo kuhakikisha vifaa hivyo vinatumika kwa malengo yaliyokusudiwa ili kuendelea kumpa matumaini Mr. Black na wafadhili wengine.

Walimu kutoka baadhi ya shule zilizopokea msaada huo wamemshukuru Mr. Black kwa msaada huo, wakisema kwamba utaenda kutatua changamoto zilizokuwepo katika shule zao huku wakimuomba aendelee na moyo huo wa majitolea kwa jamii ya Shinyanga.




 

Post a Comment

0 Comments