Ticker

6/recent/ticker-posts

MWENYEKITI WA JUMUIYA YA WAZAZI CCM MKOA WA SHINYANGA MHE. JOHN SIAGI AJIANDIKISHA KATIKA DAFTARI LA WAKAZI AHAMASISHA WANANCHI WA KUJITOKEZA KWA WINGI

Na Mapuli Kitina Misalaba

Mwenyekiti wa Jumuiya ya Wazazi wa Chama cha Mapinduzi (CCM) Mkoa wa Shinyanga, Mhe. John Siagi, amejiandikisha rasmi katika daftari la wakazi katika zoezi linaloendelea la kuandikisha wapiga kura kwa ajili ya uchaguzi wa serikali za mitaa Mwaka huu 2024.

Zoezi hilo ni sehemu muhimu ya maandalizi ya uchaguzi utakaofanyika Novemba 27, 2024.

Akizungumza baada ya kujiandikisha, Mhe. Siagi amesema kuwa ni furaha kwake kushiriki katika zoezi hilo, ambalo linahusisha wananchi wa Shinyanga na maeneo mengine nchini.

"Siku ya leo na mimi nimejitokeza kujiandikisha katika zoezi ambalo linaendelea la kupata takwimu za wakazi katika daftari la wapiga kura, hususani kwa ajili ya uchaguzi wa serikali za mitaa," amesema Siagi.

Mhe. Siagi ameelezea kuwa alikosa fursa ya kushiriki kwenye uzinduzi wa zoezi hili kutokana na kuwa na majukumu ya ziara ya Katibu Mkuu wa CCM, lakini amepata nafasi leo kuungana na familia yake katika zoezi hilo muhimu.

"Itakumbukwa wakati wa uzinduzi wa zoezi hili, sisi baadhi ya viongozi tulikuwa na ugeni wa ziara ya Katibu Mkuu wetu wa Chama cha Mapinduzi, hivyo basi leo nimepata fursa kuja kuungana na wenzangu kufanikisha zoezi hili mimi pamoja na familia yangu," ameongeza Siagi.

Kwa kuzingatia umuhimu wa zoezi hilo, Mhe. Siagi ametoa wito kwa wanachama wa CCM na wananchi wa Shinyanga kujitokeza kwa wingi ili kuhakikisha wanajiandikisha kwa wakati.

“Nitoe wito kwa wanachama wa Chama cha Mapinduzi, wananchi wenye mapenzi mema na chama chetu, lakini pia wananchi wote wa Mkoa wa Shinyanga kwa ujumla, tujitokeze kwa wingi kwa sababu tumepewa siku kumi za kutosha. Zoezi hili linakwenda mpaka tarehe 20, kwa hiyo tujitokeze kwa wingi tutumie fursa hii ili tuweze kuwachagua viongozi wetu,” amesema Mhe. Siagi.

Wakati huo huo, Mhe. Siagi  amewahimiza viongozi wa chama kuendelea kuhamasishana na kutoa elimu kwa wanachama na wananchi kuhusu umuhimu wa kujiandikisha.

"Rai yangu kwa viongozi wenzangu na wanachama wenzangu ni tuendelee kuhamasishana, tupeane elimu ili kufanikisha zoezi la uandikishaji katika daftari la wakazi,"

Uandikishaji huu unafanyika kwa siku kumi hadi Oktoba 20, 2024, na utatumika kwa wapiga kura katika uchaguzi wa serikali za mitaa unaotarajiwa kufanyika mwishoni mwa Novemba mwaka huu.

Zoezi hilo linaangaliwa kama moja ya hatua muhimu katika kuimarisha demokrasia na kuhakikisha ushiriki wa wananchi kwenye uongozi wa mitaa.

Wakazi wa Shinyanga wanahamasishwa kujitokeza kwa wingi katika siku zilizobaki ili kuweza kushiriki kikamilifu katika uchaguzi huo ambao utaamua uongozi wa serikali za mitaa kwa miaka ijayo.

 

Post a Comment

0 Comments