Ticker

6/recent/ticker-posts

MWENYEKITI WA NASIMAMA NA MAMA SHINYANGA ATOA WITO WA KUJIANDIKISHA KWENYE DAFTARI LA WAPIGA KURA

Na Mapuli Kitina Misalaba

Mwenyekiti wa taasisi ya Nasimama na Mama Mkoa wa Shinyanga, CDE. Oscar Kaijage Kaindoa, amewakumbusha wana-CCM na Watanzania kwa ujumla kuhusu umuhimu wa kujitokeza kujiandikisha kwenye daftari la wapiga kura kwa ajili ya uchaguzi wa viongozi wa serikali za mitaa, vijiji, na vitongoji unaotarajiwa kufanyika Novemba 27, 2024.

Akizungumza Misalaba Media baada ya kujiandikisha kwenye daftari la wakazi, Kaindoa amesema kwamba uchaguzi huu ni fursa muhimu kwa wananchi kushiriki moja kwa moja katika mchakato wa kuwapata viongozi watakaoleta maendeleo ya karibu zaidi kwenye jamii zao.

"Ni jukumu la kila mwananchi aliye na sifa kujiandikisha na kutumia haki yake ya kupiga kura ili kupata viongozi bora wanaoweza kusimamia masuala muhimu ya kijamii, kiuchumi na kimaendeleo katika maeneo yao," amesema Kaindoa.

Pia amewasisitiza vijana, wanawake, na makundi mengine yaliyoko pembezoni kuhakikisha wanajitokeza kwa wingi ili sauti zao ziweze kusikika kupitia sanduku la kura. Ameeleza kuwa kujiandikisha ni hatua ya kwanza kuelekea kufanikisha uchaguzi huru na wa haki.

Uandikishaji kwenye daftari la wapiga kura umeanza hivi karibuni, na Kaindoa ameongeza kuwa muda wa kufanya hivyo ni mchache, hivyo akawataka wananchi wasisubiri dakika za mwisho.

Kaindoa amehitimisha kwa kusema, "Mabadiliko tunayoyataka yanatokana na uwajibikaji wetu kama wananchi, na hatua ya kwanza ni kujiandikisha ili tupate fursa ya kuchagua viongozi wanaotufaa."

Uchaguzi wa serikali za mitaa, vijiji na vitongoji utakuwa hatua muhimu kuelekea Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2025, hivyo jitihada za kuwahamasisha wananchi kushiriki kikamilifu zinaendelea kufanywa na viongozi wa taasisi mbalimbali, ikiwa ni pamoja na Nasimama na Mama.


 

Post a Comment

0 Comments