Ticker

6/recent/ticker-posts

SMAUJATA YATOA WITO KWA WANANCHI KUJIANDIKISHA KWA WINGI, KAGUNZE:HAKUNA MUDA WA ZIADA UTAKAONGEZWA BAADA YA SIKU KUMI ZILIZOTENGWA

Na Mapuli Kitina Misalaba

Msimamizi wa uchaguzi wa serikali za mitaa, Mwalimu Alexius Kagunze, ameendelea kuhamasisha wananchi kujitokeza kwa wingi kwenye zoezi la uandikishaji wa wakazi.

Zoezi hilo limeanza rasmi tarehe 11 Oktoba 2024, na litafikia tamati tarehe 20 Oktoba 2024, likiwa na lengo la kuwaandikisha wapiga kura watakaoshiriki uchaguzi wa viongozi wa serikali za mitaa.

Kagunze ameeleza kuwa, zoezi hilo linaendeshwa kila siku kuanzia saa mbili asubuhi hadi saa kumi na moja jioni, na hakuna muda wa ziada utakaongezwa baada ya siku kumi zilizotengwa.

“Naendelea kuwasihi wananchi wote wa Halmashauri ya Manispaa ya Shinyanga kufika kwenye vituo vilivyo karibu na makazi yao ili waweze kujiandikisha. Hili ni zoezi muhimu sana, na kama hukutumia fursa hii, utapoteza haki ya kushiriki kwenye uchaguzi wa tarehe 27 Novemba 2024. Sifa kuu za kujiandikisha ni kuwa na umri wa miaka 18 na kuendelea, pamoja na kuwa mkazi wa eneo husika,” amesema Kagunze.

Naye Katibu wa jumuiya ya shujaa wa maendeleo na ustawi wa jamii Tanzania (SMAUJATA) Kanda ya Ziwa, Daniel Patrick Kapaya ameendelea kuhamasisha wananchi, hususan vijana wa mikoa ya Shinyanga, Mwanza, Mara, Simiyu, Geita, na Kagera, kujitokeza kwa wingi kujiandikisha.

“Naomba sana mashujaa wote wa kanda yangu ya Ziwa, pamoja na wananchi kwa ujumla, wajitokeze kujiandikisha kwenye daftari la wakazi. Ni haki ya msingi kwa kila mmoja kujiandikisha ili aweze kupiga kura, kwani usipojiandikisha unajinyima haki hiyo. Tarehe 27 Novemba 2024, tutakuwa na uchaguzi wa viongozi wa serikali za mitaa, ambao ndio watahakikisha maendeleo ya mitaa yetu,” amesema Kapaya.

Kapaya ameendelea kufikisha salamu za mwenyekiti wa taifa wa SMAUJATA, Sospeter Bulugu, akisisitiza kuwa mashujaa na wananchi kwa ujumla wanatakiwa kujitokeza ili kujiandikisha ambapo amewasisitiza wananchi wasikose fursa hiyo kwani ndio itakayowezesha ushiriki wao katika uchaguzi wa viongozi watakaoliongoza taifa kwa ngazi za mitaa.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Idara ya Itifaki, Uenezi, na Uanachama wa SMAUJATA Mkoa wa Shinyanga, Solomon Najulwa, ameungana na viongozi wenzake kutoa wito kwa wananchi wa Shinyanga kuhakikisha wanajiandikisha kwa wingi.

Najulwa amesema kuwa, zoezi hilo ni tofauti na ule wa kuboresha daftari la wapiga kura ambalo litatumika mwaka 2025 kwenye uchaguzi mkuu wa madiwani, wabunge, na rais.

“Zoezi hili ni la uandikishaji kwenye daftari la wakazi, halihusishi kitambulisho chochote. Unachotakiwa ni kutoa majina yako matatu, umri, na sahihi uandikishaji huu ni wa haraka, na mara tu unapomaliza, unakuwa na sifa ya kuwa mkazi halali wa eneo husika,” amesema Najulwa.

Najulwa amewahimiza wananchi, hususan wale wanaoishi na watu wenye ulemavu au wazee, kuwasaidia kufika kwenye vituo vya uandikishaji ili kuhakikisha kila mmoja anapata haki ya kushiriki uchaguzi huo.

“Kama hatutawasaidia ndugu zetu wenye ulemavu au wazee kufika kwenye vituo vya uandikishaji, tutakuwa tunafanya ukatili kwa kuwanyima haki yao ya msingi SMAUJATA tunasema, tuonyeshe upendo kwao kwa kuwahakikisha wanajiandikisha,” amesema Najulwa.

Uchaguzi wa viongozi wa serikali za mitaa utakaofanyika tarehe 27 Novemba 2024 ni mchakato muhimu kwa maendeleo ya maeneo ya mitaa.

Viongozi watakaopatikana katika uchaguzi huo watakuwa na jukumu kubwa la kusimamia maendeleo na ustawi wa jamii katika ngazi za msingi ambapo Wananchi wanahimizwa kutumia haki yao ya kidemokrasia kwa kujiandikisha na kisha kushiriki uchaguzi huo.

Wananchi wa Manispaa ya Shinyanga na mikoa mingine ya Kanda ya Ziwa wamepewa mwaliko wa kutumia siku zilizobaki kuhakikisha wanajiandikisha kwa ajili ya kupiga kura, kwani uandikishaji huu ni fursa ya kipekee kwao kuchagua viongozi watakaowaletea maendeleo.

Katibu wa jumuiya ya shujaa wa maendeleo na ustawi wa Jamii Tanzania (SMAUJATA) Kanda ya Ziwa, Daniel Patrick Kapaya, akijiandikisha kwenye daftari la wakazi.

Mwenyekiti wa Idara ya Itifaki, Uenezi, na Uanachama wa SMAUJATA Mkoa wa Shinyanga, Solomon Najulwa (Cheupe) akijiandikisha kwenye daftari la wakazi.

 

Post a Comment

0 Comments