KATA YA KITANGILI WAADHIMISHA MIAKA 48 YA CCM MJUMBE WA JUMUIYA YA WAZAZI CCM WILAYA YA SHINYANGA MJINI DANIEL KAPAYA ATOA ELIMU DHIDI YA UKATILI KWA WATOTO

Na Mwandishi wetu, Misalaba Media

Katika maadhimisho ya miaka 48 ya Chama Cha Mapinduzi (CCM), Mjumbe wa Kamati ya Utekelezaji  Jumuiya ya Wazazi Wilaya ya Shinyanga Mjini, Daniel Kapaya, amefanya ziara katika Zahanati ya Kitangili na Shule ya Msingi Kitangili, akitoa elimu juu ya kupinga ukatili dhidi ya watoto kwa kushirikiana na viongozi wa jumuiya hiyo kata na matawi.

Kapaya amewataka wazazi kufuatilia maendeleo ya watoto wao shuleni na kushiriki kuchangia chakula pamoja na sukari, akisisitiza kuwa kutofanya hivyo kunaweza kuchangia ukatili dhidi yao.

Aidha, amewatahadharisha watoto dhidi ya matumizi ya simu janja (smartphones), akieleza kuwa yanaweza kuwa chanzo cha ukatili wa mtandaoni, ikiwa ni pamoja na unyanyasaji na kudanganywa na watu wasiofaa.

Katika zahanati hiyo, Kapaya na timu yake walipanda miti na kutoa elimu kuhusu umuhimu wa usalama na ulinzi wa watoto.

Shuleni, amezungumza na wanafunzi na wazazi kuhusu madhara ya ukatili wa kijinsia, mimba za utotoni, ulawiti, ubakaji, na matumizi ya dawa za kulevya. Vilevile, alitoa kilo 50 za unga wa mahindi kusaidia lishe ya wanafunzi.

Amesisitiza kuwa wazazi wanapaswa kuchangia maendeleo ya shule badala ya kutegea, akibainisha kuwa kutofanya hivyo ni aina ya ukatili kwa watoto.

Pia, amewataka wataalamu wa afya kufanya kazi kwa weledi kwa kuzingatia miongozo na taratibu za utumishi wa umma, akisisitiza umuhimu wa utoaji wa huduma kwa usawa kwa wananchi wote.

 


 

Previous Post Next Post