" BARAZA LA MITUME NA MANABII LAZINDUA MAOMBI MAALUM SHINYANGA ‘NGUVU KUBWA KILA MAHALI’ NABII MESHACK: "MSICHANA SIYO MKE, MVULANA SIYO MUME"

BARAZA LA MITUME NA MANABII LAZINDUA MAOMBI MAALUM SHINYANGA ‘NGUVU KUBWA KILA MAHALI’ NABII MESHACK: "MSICHANA SIYO MKE, MVULANA SIYO MUME"

Na Mapuli Kitina Misalaba

Mwenyekiti wa Baraza la Makanisa ya Mitume na Manabii Kanda ya Ziwa Nabii Meshack Mpanduji, amezindua rasmi maombi maalumu yanayotambulika kwa jina la Maombi ya Nguvu Kubwa Kila Mahali.

Uzinduzi huo umefanyika katika Kanisa la Jehovah Shalom lililopo Kata ya Ndala, Manispaa ya Shinyanga.

Maombi hayo yamelenga kuimarisha huduma tano za kiroho zinazojumuisha Mitume, Manabii, Wainjilisti, Wachungaji, na Walimu wa makanisa.

Katika mahubiri yake, Nabii Meshack amewahimiza Watanzania kuepuka kufanya mambo kwa mazoea au kwa kuiga, akisisitiza kuwa mara nyingi watu wanaofanya vitu bila uelewa hufeli.

“Jambo lolote unalolifanya hakikisha unauelewa kama hauna uelewa, usilifanye. Unapotaka kuanzisha biashara yoyote, jitahidi kuielewa kwanza watu wengi wanashindwa kwa sababu wanajiingiza kwenye mambo bila kuwa na maarifa ya kutosha.”

Katika hatua nyingine, Nabii Meshack amezungumzia masuala ya ndoa na umuhimu wa kujiandaa kiakili na kiroho kabla ya kuingia kwenye ndoa.

“Kwenye kutengeneza mji, kuna msichana na mvulana, na kuna mwanamke na mwanaume. Msichana hatimizi hatima ya ndoa; anayetimiza hatima ya ndoa ni mwanamke. Maandiko yanasema mtu atamwacha baba na mama na kuambatana na mke, siyo msichana. Hali kadhalika, mvulana hatimizi hatima ya ndoa, bali mwanaume ndiye mwenye wajibu huo.”

Ameeleza kuwa migogoro mingi ya ndoa hutokea kwa sababu wanandoa huingia kwenye maisha ya ndoa wakiwa hawajajitambua vya kutosha.

“Wanaotaka kuingia kwenye ndoa, jichunguzeni kwanza. Kama wewe ni msichana, bado hujawa tayari kuwa mke. Vivyo hivyo, kama bado ni mvulana, usilazimishe kuingia kwenye ndoa.”

Baadhi ya waumini waliohudhuria uzinduzi huo wameeleza kufurahishwa na mahubiri ya Nabii Meshack, hasa katika suala la ndoa, wakisema yamewapa mwanga wa kutambua majukumu yao katika maisha ya ndoa.

Mwenyekiti wa Mitume na Manabii Mkoa wa Shinyanga, Aposto Themistocles Paul, amesema kuwa maombi hayo yatakuwa na nguvu kubwa na yatafanyika kwa vitendo.

“Kuanzia sasa, tutafanya maombi haya nyumba kwa nyumba, kanisa kwa kanisa, na kila wilaya ili kuombea wenye changamoto mbalimbali.”

Ameongeza kuwa wanatarajia kuandaa maombi maalum kwa ajili ya Uchaguzi Mkuu wa mwaka huu, ili kuombea amani ya Tanzania.

“Tunashauri watu waendelee kuwa na vyama vyao vya siasa lakini kudumisha umoja na amani. Tanzania ni nchi yetu sote, hivyo tuilinde kwa maombi.”

Katibu wa Baraza la Mitume na Manabii Mkoa wa Shinyanga, Nabii Avithi Salvatory, ambaye pia ni Kiongozi wa Kanisa la Jehovah Shalom, amesema kuwa lengo la uzinduzi wa Nguvu Kubwa Kila Mahali ni kuwafikia watu wengi na kuombea taifa pamoja na viongozi wake.

“Tutamwombea Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan, pamoja na wasaidizi wake wote ili waendelee kuongoza kwa hekima na busara.”

Maombi hayo yatajikita katika maeneo mbalimbali muhimu, ikiwemo kukemea ukatili unaoendelea katika jamii, kuombea uchumi wa taifa na ustawi wa watu binafsi, kuombea amani ya taifa, kuomba dhidi ya vitendo vya uovu vinavyofanyika kinyume cha utaratibu wa nchi.

Baraza la Makanisa ya Mitume na Manabii Tanzania (BMMMT) limeeleza kuwa na maombi hayo ambayo yataendelea kufanyika kote nchini kwa lengo la kuimarisha kiroho na kijamii.Viongozi mbalimbali wakimpokea Nabii Meshack baada ya kuwasili Mkoani Shinyanga.





 

Post a Comment

Previous Post Next Post