" JESHI LA POLISI MKOANI SHINYANGA LINAMSHIKILIA MTUHUMIWA MMOJA WA TUKIO LA MTOTO WA MIAKA 7 KUUAWA NDALA

JESHI LA POLISI MKOANI SHINYANGA LINAMSHIKILIA MTUHUMIWA MMOJA WA TUKIO LA MTOTO WA MIAKA 7 KUUAWA NDALA

Na Mapuli Kitina Misalaba

Jeshi la Polisi Mkoa wa Shinyanga linaendelea na uchunguzi wa mauaji ya mtoto Dorin Almin (7), mwanafunzi wa darasa la pili katika Shule ya Msingi Msufini, ambaye aliuawa na mtu au watu wasiojulikana katika mtaa wa Mlepa, kata ya Ndala, Manispaa ya Shinyanga.

Kamanda wa Polisi Mkoa wa Shinyanga, Kamishna Msaidizi Mwandamizi wa Polisi Janeth Magomi, amesema tukio hilo liliripotiwa mnamo Februari 11, 2025, majira ya saa 12 jioni na mzazi wa marehemu, Aminiel Benard.

"Tulipata taarifa kutoka kwa mama wa mtoto ambaye aligundua kuuawa kwa mtoto wake wa kike. Mtoto huyo alikuwa akiishi na bibi yake katika kitongoji cha Msufini, kata ya Ndala. Aliondoka kwenda shule lakini hakurejea, hali iliyopelekea bibi yake kuanza kumtafuta jioni hiyo," amesema Kamanda Magomi.

Jeshi la Polisi tayari linamshikilia mtuhumiwa mmoja wa kiume kwa ajili ya mahojiano, huku uchunguzi ukiendelea. Inadaiwa kuwa mama mzazi wa marehemu anaishi Bugweto baada ya kuolewa na mwanaume mwingine, na mmoja wa watu wanaoshikiliwa ni aliyekuwa mume wake.

"Sisi kama Jeshi la Polisi tutaendelea na upelelezi wa kina ili kubaini wahusika wa mauaji haya na kuhakikisha sheria inachukua mkondo wake," ameongeza Kamanda Magomi.

Kwa upande wao, familia ya marehemu imeeleza kusikitishwa na tukio hilo, huku wakazi wa Ndala wakilitaka Jeshi la Polisi kufanya uchunguzi wa kina ili wahusika wachukuliwe hatua kali za kisheria.

Mwenyekiti wa mtaa wa Mlepa, Abel Baziri, amesema kuwa kwa kushirikiana na jeshi la sungusungu, wamejipanga kuchukua hatua za kuimarisha ulinzi, ikiwemo kufanya doria na misako ya nyumba kwa nyumba ili kubaini wageni waliowasili kwenye mtaa huo bila taarifa rasmi kwa serikali ya mtaa.

Jeshi la Polisi linaendelea na uchunguzi ili kubaini wahusika wa tukio hilo la kikatili.

TAZAMA VIDEO

Post a Comment

Previous Post Next Post