TAKUKURU YABAINI MAPUNGUFU KWENYE MAUZO YA VIWANJA KAHAMA YAOKOA MILIONI 137.8 NA KUENDELEA KUFUATILIA SHILINGI MILIONI 600

Mkuu wa TAKUKURU Mkoa wa Shinyanga, Donasian Kessy akitoa taarifa yake kwa waandishi wa habari leo Februari 4, 2025.

Na Mapuli Kitina Misalaba

Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) Mkoa wa Shinyanga imefanikiwa kuokoa shilingi milioni 137.8 ikiwa ni sehemu ya fedha za malipo ya mauzo ya viwanja 29 vilivyopimwa na Manispaa ya Kahama mwaka 2019.

Mkuu wa TAKUKURU Mkoa wa Shinyanga, Donasian Kessy, ametoa taarifa hiyo leo wakati akielezea utekelezaji wa majukumu ya taasisi hiyo kwa kipindi cha robo ya pili ya mwaka wa fedha 2024/2025, kuanzia Oktoba hadi Desemba.

Amesema Manispaa ya Kahama ilikuwa ikimiliki ardhi katika eneo la Phantom na mwaka 2019 iliamua kupima na kuuza viwanja hivyo kwa wananchi. Hata hivyo, amesema TAKUKURU inaendelea kufuatilia malipo ya fedha zilizobaki, ambazo ni zaidi ya shilingi milioni 600.

“Mwaka 2024, TAKUKURU kupitia vyanzo vyake vya siri, ilipata taarifa kuwa baadhi ya wananchi wamemilikishwa viwanja hivyo bila kulipia gharama zilizohitajika kwa mujibu wa taratibu zilizowekwa na Manispaa hiyo”.

 “TAKUKURU imeweza kuwafikia baadhi ya waliomilikishwa viwanja hivyo na kuwataka walipie gharama za mauzo ya viwanja hivyo kama ilivyopaswa au viwanja husika vitangazwe upya ili kupata wanunuzi watakaoweza kulipia gharama husika”.

“Wamiliki waliofikiwa walikubali kufanya malipo ya viwanja hivyo kama walivyopaswa. Mpaka sasa jumla ya TZS. 137,800,000/=  kati ya TZS. 800,000,000/=  zimelipwa kwa Manispaa ya Kahama kupitia Account ya Miscellaneous Deposit”.

“Aidha TAKUKURU inaendelea kusimamia ulipwaji wa fedha zote zilizobaki ambazo ni takriban TZS. 662,200,000/=  ili kuhakikisha viwanja vyote vinalipiwa na fedha zake zinaingia Serikalini”.amesema Kessy

Katika kipindi hicho, TAKUKURU Mkoa wa Shinyanga pia imefuatilia miradi 10 ya sekta ya elimu yenye thamani ya shilingi bilioni 3.1 katika Halmashauri ya Wilaya ya Shinyanga, Kishapu na Manispaa ya Shinyanga.

Aidha, kupitia dawati la uchunguzi, taasisi hiyo imepokea malalamiko 38, ambapo 20 kati yake yanahusiana na rushwa na uchunguzi wake unaendelea, huku malalamiko 18 yakiwa hayahusiani na rushwa.

 Mkuu wa TAKUKURU Mkoa wa Shinyanga, Donasian Kessy akitoa taarifa yake kwa waandishi wa habari leo Februari 4, 2025.

 

Previous Post Next Post