UMOJA WA WANAWAKE TANZANIA (UWT) CCM KATA YA NDEMBEZI WATEMBELEA NA KUTOA MSAADA KATIKA KITUO CHA KULELEA WATOTO YATIMA BUSHUSHU

Na Elisha Petro, Misalaba Media

Umoja wa Wanawake Tanzania (UWT) Chama cha Mapinduzi CCM Kata ya Ndembezi wakiongozwa na Mwenyekiti wa Umoja huo Linah Kazimiri wametembelea kituo cha watoto yatima Bushushu Manispaa ya Shinyanga na kutoa msaada wa vitu mbalimbali ikiwa ni sehemu ya maadhimisho ya miaka 48 ya kuanzishwa kwa Chama cha Mapinduzi CCM.

Akizungumza wakati wa kukabidhi msaada huo Mwenyekiti Linah Kazimiri amewasisitiza Wajumbe wa umoja huo na jamii Kwa ujumla kujifunza kupitia kituo hicho cha watoto yatima Bushushu ili kuendelea kuwa na moyo wa majitoleo na kusaidia watu wenye uhitaji katika jamii.

"Ndugu zangu kwanza niwapongeze kwa utayari wa kufika hapa na moyo wenu wa majitoleo kuwasaidia watoto wetu lakini nimewaleta hapa ili tujifunze na jamii ijifunze kupitia sisi juu ya umuhimu wa kuguswa kusaidia makundi yenye uhitaji katika jamii zetu ikiwemo kituo hiki cha kulea watoto yatima na Kila mmoja wetu atoke hapa akijua kuwa pale unapopata kile ulichojaliwa nacho basi kumbuka kusaidia wahitaji isiishie leo tu bali iwe mwendelezo kila mara"

Awali akizungumza kabla ya kukabidhi vitu hivyo Katibu wa UWT Kata ya Ndembezi Bi. Christina Stanslaus Milenge ameushukuru uongozi wa kituo hicho kwa ushirikiano waliouonyesha na kuahidi kuwa wataendelea kushirikiana na kutenga muda wao kufika kituoni hapo ili kuwa karibu zaidi na watoto.

"Mama yetu mpendwa na mlezi wa Kituo hiki kwanza kabisa nimefarijika kwa mapokezi yenu makubwa na utayari wenu wa kutukaribisha kituoni hapa sisi UWT Kata ya Ndembezi tumefika hapa kukaa na watoto wetu lakini pia tumewaletea ridhiki hii ya vitu mbalimbali (Mchele,Vinywaji,Sabuni )  tunaomba muipokee lakini pia tunaahidi kuendelea kushirikiana na kutenga muda wetu kufika mahali hapa ili kuwafariji watoto wetu na kuwa karibu nao"

 

Kwa upande wake mmiliki wa Kituo cha kulelea watoto yatima Bushushu Bi. Ayam Ally Said maarufu kwa jina la Mama yatima amewapongeza viongozi na Wajumbe wa UWT Kata ya Ndembezi kwa msaada walioutoa na kutenga muda wao kwenda kuwafariji watoto hao na kuwaomba waendelee kuwa na Umoja ,Upendo na Mshikamano kwa lengo la kusaidia makundi yote yenye uhitaji katika jamii.

"Kwanza kabisa niwashukuru kwa Umoja wenu kwa msaada huu mkubwa lakini pia  kufika katika kituo chetu na kuwasalimia watoto wenu naamini Mwenyezi Mungu atawazidishia mlipogusa lakini niwaombe sana mwendelee kudumisha Umoja huu mpendane na kuvumiliana katika kila hali najua sisi wakina mama tunanafasi kubwa katika malezi ya watoto hawa niwaombe isiishie tu leo kwa sababu ni maadhimisho ya CCM sisi milango yetu ipo wazi kila wakati mje kuwasalimia watoto hawa sio lazima uje na kitu cha kushikika hata neno lako ni faraja tosha naomba sana msirudi nyuma muendelee na Umoja huu" 

Wakizungumza na Misalaba Media baadhi ya watoto katika kituo hicho wameshukuru kwa msaada waliopokea kutoka UWT Kata ya Ndembezi na kufanya Dua ya kushukuru na kuwaombea wote walioguswa na kutoa msaada huo huku wakiwaomba waendelee kuwa na moyo wa majitoleo.

 

Hafla hiyo imetanguliwa na zoezi la upandaji wa miti ambapo viongozi mbalimbali wa Chama cha Mapinduzi CCM Kata ya Ndembezi wamehudhuria mwanzo hadi mwisho wa zoezi hilo ikiwa ni sehemu ya maadhimisho ya miaka 48 ya kuanzishwa kwa Chama cha Mapinduzi CCM ambapo kilele chake ni tarehe 05.2.2025

 

Previous Post Next Post