Na Mapuli Kitina Misalaba
Umoja wa Wanawake wa Chama cha Mapinduzi (UWT) Mkoa
wa Shinyanga umeadhimisha miaka 48 ya CCM kwa kufanya matendo ya huruma,
ikiwemo kutoa msaada kwa wagonjwa hospitalini na katika kituo cha afya, pamoja
na kupanda miti ili kuunga mkono juhudi za serikali katika utunzaji wa
mazingira.
Sherehe hizo kwa ngazi ya Mkoa zimefanyika katika
Wilaya ya Shinyanga Vijijini Februari 1, 2025 ambapo wanachama na viongozi wa UWT wameshiriki
zoezi la upandaji miti katika eneo la nyumba ya Katibu wa UWT wilayani humo.
Aidha, jumuiya hiyo imetoa msaada wa sabuni za unga
na vipande, mafuta ya kujipaka, pamoja na juisi kwa wagonjwa waliolazwa katika
Hospitali ya Wilaya ya Shinyanga Vijijini, wakiwemo walioko katika wodi ya
wazazi.
Katika hatua nyingine, UWT pia imetoa msaada wa
mashuka kwa wagonjwa katika kituo cha Afya Nindo, ambapo msaada huo ni sehemu
ya maadhimisho ya miaka 48 tangu kuanzishwa kwa CCM.
Akizungumza katika hafla hiyo, Mwenyekiti wa UWT
Mkoa wa Shinyanga, Bi. Grace Samweli Bizuru, amesema kuwa wanawake wa UWT
wanajivunia kuwa sehemu ya CCM kwa sababu chama hicho kinaendelea kuleta
maendeleo chanya kila wakati.
Amewahimiza wananchi kuendelea kukiunga mkono chama
hicho pamoja na viongozi wa serikali katika utekelezaji wa Ilani ya CCM ili
kero na changamoto zinazowakabili wananchi ziweze kutatuliwa kwa ufanisi.
Aidha, Bi. Bizuru amesisitiza kuwa UWT Mkoa wa
Shinyanga inaunga mkono uamuzi wa Mkutano Mkuu wa CCM wa kumpitisha Mhe. Samia
Suluhu Hassan kuwa mgombea wa urais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ambapo
amebainisha kuwa jumuiya hiyo itaendelea kusimama bega kwa bega na Rais Samia
kuhakikisha anapata ushindi mkubwa katika uchaguzi ujao.
Katika hotuba yake, Bi. Bizuru pia amewahimiza
wanawake kuimarisha malezi bora kwa watoto wao ili waweze kukua katika misingi
ya maadili mema huku akitoa wito kwa wanawake kupaza sauti dhidi ya vitendo vya
ukatili vinavyowakumba wanawake na watoto ili hatua za kisheria zichukuliwe kwa
wahusika.
Kwa upande wake, Mgeni mwalikwa katika maadhimisho
hayo, Mjumbe wa Halmashauri Kuu ya CCM Wilaya ya Kahama na Mjumbe wa Kamati ya
Siasa Mkoa wa Shinyanga, Simon Makoye Mayengo, ameipongeza Serikali ya awamu ya
Sita chini ya uongozi wa Rais Samia Suluhu Hassan kwa utekelezaji mzuri wa
Ilani ya CCM.
“Chama
cha Mapinduzi kinafanya kazi kubwa chini ya Rais Samia Suluhu Hassan. Katika
Mkoa wetu wa Shinyanga, tumeshuhudia ongezeko kubwa la miradi ya maendeleo,
ikiwemo ujenzi wa barabara za lami, madaraja, vituo vya afya na miundombinu
mingine muhimu. Hatuna sababu ya kushindwa kumpa kura nyingi Rais wetu Samia
Suluhu Hassan ili aendelee kutuletea maendeleo,”
amesema Mayengo.
Amemalizia kwa kuwasihi wanachama wa CCM na wananchi
kwa ujumla kuhakikisha wanajitokeza kwa wingi wakati wa uchaguzi ili kumpa
ushindi wa kishindo Mhe. Samia Suluhu Hassan.
Maadhimisho hayo yameacha alama ya upendo na
mshikamano miongoni mwa wanajumuiya wa UWT na jamii kwa ujumla, huku
yakionyesha dhamira ya CCM katika kuboresha maisha ya wananchi na kulinda
mazingira kwa vizazi vijavyo.
Mwenyekiti wa UWT Mkoa wa Shinyanga, Bi. Grace
Samweli Bizuru, akikabidhi zawadi ikiwa ni sehemu ya maadhimisho ya Miaka 48 ya
CCM.
Mgeni mwalikwa katika maadhimisho hayo, Mjumbe wa
Halmashauri Kuu ya CCM Wilaya ya Kahama na Mjumbe wa Kamati ya Siasa Mkoa wa
Shinyanga, Simon Makoye Mayengo, akikabidhi zawadi.
Mwenyekiti wa UWT Mkoa wa Shinyanga, Bi. Grace
Samweli Bizuru, akipanda mti katika eneo la nyumba ya katibu wa UWT Wilaya ya
Shinyanga vijijini.
Mwenyekiti wa UWT Mkoa wa Shinyanga, Bi. Grace
Samweli Bizuru, akipanda mti katika eneo la nyumba ya katibu wa UWT Wilaya ya
Shinyanga vijijini.
Mgeni mwalikwa katika maadhimisho hayo, Mjumbe wa
Halmashauri Kuu ya CCM Wilaya ya Kahama na Mjumbe wa Kamati ya Siasa Mkoa wa
Shinyanga, Simon Makoye Mayengo, akipanda mti.
Mgeni mwalikwa katika maadhimisho hayo, Mjumbe wa
Halmashauri Kuu ya CCM Wilaya ya Kahama na Mjumbe wa Kamati ya Siasa Mkoa wa
Shinyanga, Simon Makoye Mayengo, akizungumza.
Mgeni mwalikwa katika maadhimisho hayo, Mjumbe wa
Halmashauri Kuu ya CCM Wilaya ya Kahama na Mjumbe wa Kamati ya Siasa Mkoa wa
Shinyanga, Simon Makoye Mayengo, akizungumza.
Mwenyekiti wa UWT Mkoa wa Shinyanga, Bi. Grace Samweli Bizuru, akikabidhi zawadi kwa wawakilisha wa kituo cha Afya Nindo.