" WATU 1,349 MKOANI SHINYANGA WAKADIRIWA KUWA NA KIFUA KIKUU WANANCHI WAHIMIZWA KUPIMA

WATU 1,349 MKOANI SHINYANGA WAKADIRIWA KUWA NA KIFUA KIKUU WANANCHI WAHIMIZWA KUPIMA

Na Mapuli Kitina Misalaba

Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga, Mhe. Anamringa Macha, ameongoza uzinduzi wa kampeni maalum ya kuibua na kuwafikia wananchi wenye vimelea vya ugonjwa wa kifua kikuu (TB) ambao bado hawajafikiwa na huduma za uchunguzi na matibabu.

Kampeni hiyo inafanyika bure kwa wananchi wote, ikiwa na lengo la kutokomeza mzunguko wa maambukizi ya TB katika jamii ya Shinyanga.

Mganga Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga, Dkt. Yudas Ndungile, amesema kampeni hiyo inalenga kufanikisha upimaji wa watu takribani 1,349, idadi inayokadiriwa kuwa na maambukizi kwa mujibu wa takwimu za viashiria vya ugonjwa huo.

"Hii ni kampeni harakishi ya kuibua na kuwafikia wananchi wote wenye vimelea vya kifua kikuu na ambao hawajawahi kufikiwa. Kampeni hii itakuwa bure, wananchi wanakaribishwa kupima, na wale watakaogundulika na ugonjwa watapatiwa matibabu bure. Lengo letu ni kuhakikisha hakuna mzunguko wa maambukizi ya kifua kikuu katika jamii ya Mkoa wa Shinyanga," amesema Dkt. Ndungile.

Kwa upande wake, Mganga Mfawidhi wa Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Shinyanga, ambaye pia ni Daktari Bingwa wa Magonjwa ya ndani, Dkt. Luzila John, ameeleza kuhusu ugonjwa wa kifua kikuu, akibainisha kuwa ni maradhi yanayoambukizwa kwa njia ya hewa na yamesababisha vifo vya watu milioni 2.5 kwa mwaka 2023 duniani, kwa mujibu wa Shirika la Afya Duniani (WHO).

"Tafiti zinaonesha kuwa asilimia 25 ya watu tayari wana maambukizi ya wadudu wa TB, ingawa si wote wanaougua mara moja. Dalili kuu za ugonjwa huu ni kikohozi cha muda mrefu, homa za mara kwa mara, kupungua uzito, kutoka jasho usiku na dalili nyingine zinazotegemea sehemu iliyoathirika mwilini," amesema Dkt. Luzila.

Baadhi ya wananchi waliojitokeza kwenye uzinduzi huo wameeleza kufurahishwa na huduma hiyo kutolewa bure, huku wakiwataka wataalamu wa afya kuhakikisha kuwa inawafikia wananchi wengi kwa ubora unaotakiwa.

Uzinduzi huo umefanyika katika Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Shinyanga Mwawaza, na kuhudhuriwa na viongozi mbalimbali wakiwemo Waganga Wakuu wa Halmashauri zote sita za Shinyanga, Wakurugenzi wa Halmashauri, viongozi wa dini, Mstahiki Meya wa Manispaa ya Shinyanga Mhe. Elias Ramadhan Masumbuko, pamoja na Mwenyekiti wa CCM Wilaya ya Shinyanga Mhe. Anord Makombe.

Wananchi wanahimizwa kujitokeza kwa wingi kupima na kupata matibabu ili kusaidia juhudi za kutokomeza ugonjwa wa kifua kikuu katika Mkoa wa Shinyanga.

Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga, Mhe. Anamringa Macha akizindua kampeni maalum ya kuibua na kuwafikia wananchi wenye vimelea vya ugonjwa wa kifua kikuu (TB) katika Mkoa wa Shinyanga.

Mganga Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga, Dkt. Yudas Ndungile akieleza malengo ya kampeni hiyo.

Mganga Mfawidhi wa Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Shinyanga, ambaye pia ni Daktari Bingwa wa Magonjwa ya ndani, Dkt. Luzila John, ameeleza kuhusu ugonjwa wa kifua kikuu.
Viongozi mbalimbali.



Post a Comment

Previous Post Next Post