" WATU ZAIDI YA 8,000 WAPIMWA TB, WAGONJWA 464 WA KIFUA KIKUU WABAINIKA MKOANI SHINYANGA

WATU ZAIDI YA 8,000 WAPIMWA TB, WAGONJWA 464 WA KIFUA KIKUU WABAINIKA MKOANI SHINYANGA

Na Mapuli Kitina Misalaba

Kampeni harakishi ya upimaji wa ugonjwa wa kifua kikuu (TB) inaendelea mkoani Shinyanga, ambapo hadi kufikia Februari 10, 2025, wagonjwa 464 wamebainika kati ya lengo la wagonjwa 1,349.

Akizungumza na Misalaba Media, Mratibu wa Kifua Kikuu na Ukoma Mkoa wa Shinyanga Dkt. Laurent Mhembe, amesema kampeni hiyo inahusisha Halmashauri zote sita za Mkoa huo, ambapo jumla ya vituo 72 vimeshiriki kikamilifu.

"Katika zoezi hili, kila Halmashauri tumetambua vituo 12, hivyo tumekuwa na vituo 72 vinavyotoa huduma kila kituo kilikuwa na wahudumu wa afya wawili, hivyo jumla ya wahudumu 144 wa ngazi ya jamii walihusika katika kampeni hii," amesema Dkt. Mhembe.

Kwa mujibu wa Dkt. Mhembe, takwimu za mwaka jana zilionyesha kuwa baadhi ya Halmashauri hazikufikia malengo ya kubaini idadi ya wagonjwa waliotarajiwa. Hali hiyo ilikuwa kama ifuatavyo:

Halmashauri ya Kahama - upungufu wa wagonjwa 143

Halmashauri ya Kishapu - upungufu wa wagonjwa 140

Halmashauri ya Msalala - upungufu wa wagonjwa 241

Shinyanga Vijijini - upungufu wa wagonjwa 205

Halmashauri ya Manispaa ya Shinyanga - upungufu wa wagonjwa 490

Halmashauri ya Ushetu - upungufu wa wagonjwa 130

Hali hiyo ilisababisha upungufu wa wagonjwa 1,049 kutambuliwa mwaka jana, hivyo kuhitaji juhudi za ziada mwaka huu na kwamba kampeni inayoendelea sasa, jumla ya watu zaidi ya 8,000 tayari wamepimwa, na wagonjwa 464 wamebainika na kuanza kutumia dawa.

Baadhi ya wananchi waliojitokeza kupima wameishukuru serikali kwa kutoa huduma hiyo bure, huku wakiwataka wenzao kujitokeza kwa wingi ili kupata vipimo na matibabu kwa wakati.

Kampeni hii inaendelea mkoani Shinyanga kwa lengo la kuongeza uelewa kuhusu ugonjwa wa kifua kikuu na kuhakikisha wagonjwa wanapatikana mapema ili kupata matibabu stahiki.

 

Post a Comment

Previous Post Next Post