" BIBI AFARIKI USIKU MWILI WAKE WAKUTWA ASUBUHI MTAA WA DOME SHINYANGA

BIBI AFARIKI USIKU MWILI WAKE WAKUTWA ASUBUHI MTAA WA DOME SHINYANGA

Mwanamke anayefahamika kwa jina la Anna Masele, anayekadiriwa kuwa na umri wa miaka 70, amekutwa amefariki dunia ndani ya chumba chake asubuhi ya leo katika Mtaa wa Dome, Kata ya Ndembezi, Manispaa ya Shinyanga.

Taarifa za tukio hilo zimetolewa na Mwenyekiti wa mtaa huo, Solomon Nalinga Najulwa maarufu kama Cheupe, wakati akizungumza na Misalaba Media ambaye amesema alipokea simu kutoka kwa msamaria mwema aliyetoa taarifa kuhusu kifo hicho leo Machi 8, 2025.

Kwa mujibu wa wajukuu wa marehemu, usiku wa kuamkia leo walikula chakula cha pamoja na bibi yao, ambaye hakuwa na tatizo lolote la kiafya. Baada ya chakula, kila mmoja alielekea kulala, huku marehemu akifunga mlango wa chumba chake kwa ndani kama kawaida.

“Nilipigiwa simu na msamaria mwema akiniambia kuwa kuna bibi anayedhaniwa kuwa amefariki dunia katika mtaa wangu. Nilichukua hatua ya kutoa taarifa kwa Jeshi la Polisi kisha nikaenda kwenye eneo la tukio na kujiridhisha kuwa kweli mama huyo alikuwa amefariki akiwa ndani ya nyumba yake,” amesema Najulwa.

 “Asubuhi walipoamka walimgongea mlango ili amfungulie, lakini hakujibu. Walipoona hali si ya kawaida, walikubaliana kubomoa sehemu ya mlango ili mmoja wao apite ndani, ndipo walipomkuta bibi yao akiwa tayari amefariki dunia,” ameongeza Najulwa.

Jeshi la Polisi lilifika eneo la tukio na baada ya kufanya uchunguzi wa awali, lilichukua mwili wa marehemu na kuupeleka hospitalini kwa taratibu zaidi.

Mpaka sasa mwili wa Anna Masele upo mochwari huku ndugu wakiendelea na maandalizi ya mazishi.

MISALABA MEDIA: Tutaendelea kufuatilia taarifa zaidi kuhusu tukio hili.

Post a Comment

Previous Post Next Post