" JESHI LA POLISI SHINYANGA LACHUNGUZA MAUAJI YA AGATHA ALIYEVAMIWA AKIELEKEA KANISANI

JESHI LA POLISI SHINYANGA LACHUNGUZA MAUAJI YA AGATHA ALIYEVAMIWA AKIELEKEA KANISANI

Mwanamke mmoja aitwaye Agatha Daniel Nyahuma mwenye umri wa Miaka 32, mkazi wa kijiji cha Bugayambelele, amefariki dunia baada ya kushambuliwa kwa kukatwa na kitu chenye ncha kali na mtu au watu wasiojulikana.

Akizungumza na Misalaba Media, Kaimu Kamanda wa Polisi Mkoa wa Shinyanga, ACP Kennedy Mgani, amesema tukio hilo limetokea mnamo Machi 9, 2025, majira ya saa 12 asubuhi katika mtaa wa Sido, eneo la Buhangija, kata ya Ibinzamata, Manispaa ya Shinyanga.

Kwa mujibu wa ACP Mgani, siku ya tukio, marehemu alikuwa akielekea kanisani alfajiri wakati alipovamiwa na kukatwa mgongoni chini ya bega la kulia ambapo baada ya shambulio hilo, mtuhumiwa alikimbia huku majeruhi akianguka chini.

"Majeruhi aliokolewa na wasamaria wema na kukimbizwa hospitalini kwa ajili ya matibabu, lakini kutokana na kuvuja damu nyingi, alifariki dunia akiwa hospitalini," amesema ACP Mgani.

Ameongeza kuwa mpaka sasa jeshi la polisi linaendelea na uchunguzi wa tukio hilo na kuna watu wanaotiliwa shaka, ingawa bado hawajatajwa rasmi.

ACP Mgani ametoa wito kwa wananchi wa Shinyanga kuepuka kujichukulia sheria mkononi na badala yake kufuata taratibu za kisheria katika kutatua migogoro yao.

"Endapo kuna mgogoro wowote, wananchi wasitumie njia zisizo halali. Kuna vyombo vya sheria kama mahakama na mabaraza ya ardhi ambavyo vinaweza kusaidia utatuzi wa migogoro hiyo," amesisitiza.

Jeshi la polisi linaendelea na msako wa waliohusika na tukio hilo, huku likitoa rai kwa yeyote mwenye taarifa kusaidia uchunguzi.

Post a Comment

Previous Post Next Post