" JESHI LA POLISI SHINYANGA LAWASHIKILIA WATU WAWILI KWA TUHUMA ZA MAUAJI

JESHI LA POLISI SHINYANGA LAWASHIKILIA WATU WAWILI KWA TUHUMA ZA MAUAJI

Jeshi la Polisi Mkoa wa Shinyanga linawashikilia watu wawili kwa tuhuma za mauaji ya Ndani Kasuma mwenye umri wa Miaka 72, mkazi wa kijiji cha Idodoma, kata ya Samuye, Halmashauri ya Wilaya ya Shinyanga.

Kaimu Kamanda wa Polisi Mkoa wa Shinyanga, ACP Kennedy Mgani, amesema tukio hilo limetokea Machi 3, 2025, majira ya saa tatu kuelekea saa nne usiku, wakati marehemu akiwa nje ya nyumba yake akipata chakula cha usiku na binti yake.

"Walivamiwa na watu waliokuwa na silaha zenye ncha kali, ambapo marehemu alijeruhiwa kichwani na kisogoni. Ingawa waliwatambua kwa sura, washambuliaji walikimbia baada ya kufanya tukio hilo. Jitihada za kumuwahisha hospitalini hazikufua dafu, kwani alifariki usiku huo huo," amesema ACP Mgani.

Ameeleza kuwa uchunguzi wa awali umebaini kuwa mgogoro wa ardhi huenda ndiyo chanzo cha tukio hilo, kwani marehemu alikuwa na mgogoro na watu hao hadi kufikia hatua ya kufungua mashauri katika baraza la ardhi la wilaya.

"Watu wawili tayari tumewashikilia na tunaendelea kuwasaka wengine waliohusika. Tutahakikisha wote wanakamatwa na kufikishwa kwenye vyombo vya sheria," amesema.

Jeshi la Polisi limewataka wananchi wa Mkoa wa Shinyanga kufuata taratibu za kisheria katika kutatua migogoro yao badala ya kujichukulia sheria mkononi.

Post a Comment

Previous Post Next Post