" KONGAMANO LA MISA-TAN 2025 LAWEKA MAAZIMIO MUHIMU, TAASISI ZA HABARI ZAHIMIZWA KUIMARISHA UANDISHI WA HABARI ZA MAENDELEO

KONGAMANO LA MISA-TAN 2025 LAWEKA MAAZIMIO MUHIMU, TAASISI ZA HABARI ZAHIMIZWA KUIMARISHA UANDISHI WA HABARI ZA MAENDELEO


Na Mapuli Kitina Misalaba

Waandishi wa habari nchini wametakiwa kuzingatia misingi ya taaluma yao, weledi na maadili katika kutekeleza majukumu yao, hasa katika kuelekea uchaguzi mkuu.

Mwakilishi wa Mkuu wa Mkoa wa Dodoma, ambaye pia ni Mkurugenzi Msaidizi wa Ofisi ya Taifa ya Mashtaka, Renatus Mkude, amesema hayo leo Machi 14, 2025, katika Mkutano wa Wadau wa Taasisi ya Vyombo vya Habari Kusini mwa Afrika, Tawi la Tanzania (MISA-TAN), uliofanyika jijini Dodoma.

Mkude amesisitiza umuhimu wa waandishi wa habari kutumia kalamu zao kwa uadilifu na kuzingatia misingi ya taaluma kwa manufaa ya jamii na ustawi wa taifa. "Ni wajibu wa kila mwandishi kuhakikisha kuwa habari zinazoripotiwa zinazingatia ukweli, usahihi na maadili ya taaluma ya habari," amesema.

Moja ya maazimio ya kongamano hilo ni kuhakikisha kuwa vyombo vya habari vinaanza kuzingatia habari za maendeleo na kuimarisha ushirikiano na wadau mbalimbali.

Kongamano hilo limependekeza kuanzishwa kwa vituo maalum vya mafunzo kwa waandishi wa habari kuelekea uchaguzi mkuu, ili kuwaandaa kwa weledi katika kuripoti habari za uchaguzi.

Pia tasnia ya habari inapaswa kuanza mchakato wa kuripoti habari za uchaguzi mapema – kabla, wakati na baada ya uchaguzi huku Sauti za wananchi zinapaswa kupewa kipaumbele katika habari za uchaguzi.

Aidha, MISA-TAN imetakiwa kuandaa semina maalum kwa waandishi wa habari kuhusu masuala ya uchaguzi, huku kila klabu za waandishi wa habari nchini zikihimizwa kuunda timu maalum za kuripoti habari za uchaguzi.

Katika kuhakikisha waandishi wanatekeleza majukumu yao kwa uhuru, Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA) imependekezwa kufanya mazungumzo na Jeshi la Polisi ili kuweka utaratibu wa kulinda haki za wanahabari wakati wa uchaguzi.

Katika mkutano huo, Mfuko wa Hifadhi ya Jamii kwa Watumishi wa Umma (PSSSF) umeeleza namna unavyoendelea kuimarisha mchango wake katika kukuza uchumi wa taifa kwa kuboresha uwekezaji wake.

Mwanasheria Mkuu wa PSSSF, Valentino Maganga, amesema mfuko huo umeongeza kiwango cha maendeleo kutoka asilimia 22 mwaka 2023 hadi asilimia 36 mwaka 2024/2025, huku ukilenga kufikia asilimia 40 kwa ajili ya kuimarisha uchumi wa Tanzania.

Maganga amesema PSSSF imeongeza thamani ya uwekezaji wake kutoka trilioni 6 hadi trilioni 10, huku dhamana za uwekezaji zilizopo kwenye taasisi za kifedha kama benki na majumba, zenye thamani ya Shilingi Trilioni 9, zikichangia katika ukuaji wa uchumi wa taifa.

"PSSSF inalipa pensheni kwa wastafu kila mwezi kiasi cha Shilingi Bilioni 70, na kwa mwaka ni zaidi ya Shilingi Bilioni 800. Fedha hizi huchochea shughuli za uchumi na kusaidia katika uwekezaji unaoingizia mapato serikali," amesema Maganga.

Meneja wa Kitengo cha Utangazaji wa Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA), Mhandisi Andrew Kisaka, amewataka waandishi wa habari na vyombo vya habari kuzingatia maadili ya uandishi na utangazaji, hasa wakati wa kuelekea uchaguzi mkuu.

Akizungumza katika kongamano hilo, Mhandisi Kisaka amesema vyombo vya habari vinapaswa kufanya kazi kwa haki, usawa na uadilifu, na kuhakikisha kuwa vyama vyote vya siasa vinapewa nafasi sawa katika kuripotiwa.

"Ni muhimu kwa waandishi wa habari kutenda haki kwa kuripoti kile kilichotokea kama kilivyokuwa, bila kuongeza chumvi au kufanya utani kwenye habari. Vyombo vya habari vina wajibu wa kuhakikisha wananchi wanapata taarifa sahihi na zinazowawezesha kufanya maamuzi ya busara," amesema Kisaka.

Pia amesisitiza kuwa waandishi wanapaswa kuepuka kuripoti habari zisizo za kweli na badala yake wajikite zaidi katika kuripoti sera na ahadi za vyama vya siasa, ili kuwasaidia wananchi kuelewa mipango ya vyama na jinsi wanavyokusudia kutatua changamoto zilizopo.

Mwenyekiti wa Taasisi ya Vyombo vya Habari Kusini mwa Afrika – Tanzania (MISA-TAN), Edwin Soko, amewashukuru wadau wa habari na taasisi mbalimbali kwa kufanikisha mkutano huo.

Miongoni mwa taasisi zilizojitokeza kufadhili mkutano huo ni Mfuko wa Taifa wa Hifadhi ya Jamii (NSSF), Mfuko wa Hifadhi ya Jamii kwa Watumishi wa Umma (PSSSF), Mfuko wa Bima ya Afya (NHIF), Mfuko wa Maendeleo ya Jamii (TASAF), Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA), na Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (PCCB).

Taasisi nyingine ni Shirika la TASHICO, Tanzania Human Rights Defenders Coalition (THRDC), na Pan-African Constructive Journalism Initiative (PACJI), ambazo ushiriki wao unatarajiwa kuleta mchango mkubwa katika kuboresha tasnia ya habari nchini.

Wakati huo huo Taasisi ya Vyombo vya Habari Kusini mwa Afrika, Tawi la Tanzania (MISA-TAN), imewatunuku tuzo za heshima wajumbe wa bodi waliomaliza muda wao kama ishara ya kutambua mchango wao katika uongozi wa taasisi hiyo.

Bodi hiyo iliyomaliza muda wake ilihudumu kwa miaka minane hadi uchaguzi wa viongozi wapya uliofanyika Desemba 4, 2024, ambapo Edwin Soko alichaguliwa kuwa Mwenyekiti mpya wa MISA-TAN.

Miongoni mwa waliotunukiwa ni Salome Kitomari (Mwenyekiti wa zamani), James Malenga (Makamu Mwenyekiti), pamoja na wajumbe Mussa Juma, Michael Gwimila, na Idda Mushi.

Aidha, katika mkutano huo, MISA-TAN pia imetoa vyeti vya pongezi kwa wadau wake wakuu, wakiwemo PSSSF, NSSF, TCRA, PCCB, TASAF, TASHICO, NHIF, THRDC, na PAN-AFRICAN, kwa mchango wao katika kuimarisha sekta ya habari nchini.

 

 Mwenyekiti wa Taasisi ya Vyombo vya Habari Kusini mwa Afrika  Tawi la Tanzania (MISA - TAN) , Edwin Soko akizungumza wakati Mkutano wa Misa Tanzania na wadau (MISA-TAN - Wadau Summit 2025) leo Machi 14, 2025, jijini Dodoma.











 


TAZAMA VIDEO

 

🥃🍶 TUMIA VINYWAJI BORA VYA EAST AFRICAN SPIRITS – BEI RAFIKI, LADHA SAFI BILA HARUFU MBAYA! 🍷🍸

 

Post a Comment

Previous Post Next Post