" MZEE IDD MPYALIMI: “VIUNGO VYA ALBINO HAVILETI UTAJIRI, HUU NI UDANGANYIFU”

MZEE IDD MPYALIMI: “VIUNGO VYA ALBINO HAVILETI UTAJIRI, HUU NI UDANGANYIFU”

Na Mapuli Kitina Misalaba

Kifuatia tukio la Mwanamke mwenye ualbino, Wande Mbiti Kulwa (38), mkazi wa kijiji cha Nhelegani, kata ya Kizumbi, Manispaa ya Shinyanga, kukutwa amefariki dunia ndani ya nyumba yake huku mlango ukiwa umefungwa kwa kufuli nje, ambapo hali hiyo inazua maswali kuhusu mazingira ya kifo chake.

Tukio hilo limeibua taharuki miongoni mwa wakazi wa eneo hilo, huku vikosi vya usalama vikiendelea na uchunguzi wa kina kubaini kilichotokea.

Akizungumza na Misalaba Media, aliyewahi kuwa mwenyekiti wa chama cha waganga wa tiba asili Mkoa wa Shinyanga Mzee Idd Mpyalimi, ameeleza kuwa imani za baadhi ya watu kuhusisha viungo vya watu wenye ualbino na utajiri ni potofu na zinachochewa na umaskini pamoja na udanganyifu wa waganga matapeli.

“Nimefanya utafiti kwa muda mrefu na kubaini kuwa hakuna biashara yoyote inayohusiana na viungo vya watu wenye ualbino. Ni imani potofu zinazochangiwa na hali ngumu ya maisha, ambapo watu wengi huaminishwa uongo na kuishia kupoteza pesa zao. Waganga wa tiba asili halali hawawezi kuhusika na upuuzi kama huo,” amesema Mzee Mpyalimi.

Aidha, amewataka wananchi kutoamini maneno ya matapeli wanaodai kuwa viungo vya watu wenye ualbino vinaweza kuleta utajiri. “Mganga wa tiba asili akikwambia ufanye hivyo, huyo ni tapeli, ni bora ukamlipoti polisi,” ameongeza.

Hadi sasa, jeshi la polisi mkoani Shinyanga linaendelea na uchunguzi wa kifo cha Wande Mbiti Kulwa ili kubaini chanzo cha tukio hilo.

Post a Comment

Previous Post Next Post