" SHINYANGA YAJIPANGA KUKABILIANA NA UGONJWA WA HOMA YA NYANI, WANANCHI WATAKIWA KUCHUKUA TAHADHARI

SHINYANGA YAJIPANGA KUKABILIANA NA UGONJWA WA HOMA YA NYANI, WANANCHI WATAKIWA KUCHUKUA TAHADHARI

Na Mapuli Kitina Misalaba

Daktari Godfrey Maige kutoka Idara ya Magonjwa ya Ndani katika Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Shinyanga amewatoa hofu wananchi kuhusu ugonjwa wa homa ya nyani (Mpox), akisisitiza kuwa hakuna mgonjwa aliyethibitishwa kuwa na ugonjwa huo katika hospitali hiyo hadi sasa.

Ameyasema hay oleo Machi 19, 2025 wakati akiwasilisha mada ya ugonjwa huo kwa watumishi katika Hospitali hiyo ambapo pamoja na mambo mengine amesema ugonjwa wa homa ya nyani husababishwa na virusi vinavyoitwa virusi vya nyani, ambavyo kwa mara ya kwanza viligunduliwa kwa nyani.

Amesema kuwa mgonjwa mwenye ugonjwa huu huanza kupata dalili kati ya siku ya kwanza hadi ya tano, dalili zinazofanana na mafua kama vile homa, maumivu ya misuli, na uvimbe wa tezi hasa kwenye shingo.

“Dalili nyingine ni vipele vinavyoanzia usoni na kusambaa mwilini, ambavyo baadaye hugeuka vidonda,” amesema Dkt. Maige.

Hata hivyo, Dkt. Maige ameeleza kuwa ugonjwa huo unaweza kushindwa na kinga ya mwili bila hata ya matibabu maalum ambapo ameeleza kuwa hadi sasa hakuna mgonjwa yeyote aliyethibitishwa kuwa na homa ya nyani katika Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Shinyanga, hivyo wananchi wasiwe na hofu.

“Niwatoe hofu wananchi wa Mkoa wa Shinyanga na maeneo jirani kwamba siyo kila mtu mwenye vipele ana homa ya nyani. Pia niwasihi wananchi kupata taarifa kutoka vyanzo vya kuaminika na kushirikiana na mamlaka kama ofisi ya Mganga Mkuu wa Mkoa kwa maelezo sahihi,” amesema Dkt. Maige.

Kwa upande wake, Mganga Mfawidhi wa Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Shinyanga, Dkt. Luzila John, amewataka watumishi wa afya kuwa tayari na kujiamini zaidi pasipo kuwa na hofu katika kukabiliana na ugonjwa huo.

Aidha, amebainisha kuwa Hospitali hiyo imejipanga kikamilifu kwa ajili ya kutoa huduma endapo mgonjwa yeyote atabainika kuwa na ugonjwa huo. “Tunalo eneo la kuwahifadhi wagonjwa wanaoshukiwa kuwa na homa ya nyani, na tutawahudumia kwa kushirikiana na mamlaka husika,”

Wananchi wametakiwa kuwa waangalifu na kuchukua tahadhari kwa kuepuka kugusana na mtu anayeshukiwa kuwa na dalili za ugonjwa huo, kutochukua vitu alivyogusa, na kuhakikisha wananawa mikono mara kwa mara ili kuepuka maambukizi.

Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Shinyanga inaendelea kufuatilia kwa karibu hali ya maambukizi ya homa ya nyani na kuwahimiza wananchi kufika kwenye vituo vya afya endapo watapata dalili zinazoshukiwa kuwa za ugonjwa huo.

 

Daktari Godfrey Maige kutoka Idara ya Magonjwa ya Ndani katika Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Shinyanga akiwasilisha mada ya ugonjwa wa homa ya nyani (Mpox) leo Machi 19, 2025.

Daktari bingwa wa Magonjwa ya dharura Dkt. Patrick Venance akizungumza.

Mganga Mfawidhi wa Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Shinyanga, Dkt. Luzila John, akizungumza leo Machi 19, 2025.


 

Post a Comment

Previous Post Next Post