" ALIYESAFIRI KWA BAISKELI KUTOKA KASULU HADI DODOMA KUUNGA MKONO JUHUDI ZA RAIS SAMIA SULUHU HASSAN AFANYA SAFARI NYINGINE

ALIYESAFIRI KWA BAISKELI KUTOKA KASULU HADI DODOMA KUUNGA MKONO JUHUDI ZA RAIS SAMIA SULUHU HASSAN AFANYA SAFARI NYINGINE

 

                                                                    

Na Respice Swetu, Misalaba Media -Kasulu

Mkazi wa halmashauri ya mji wa Kasulu Wencheslaus Luyaga maarufu kwa jina la Gadafi ambaye mwishoni mwa mwaka jana alisafiri kwa kutumia usafiri wa baiskeli kutoka Kasulu hadi Dodoma kuunga mkono juhudi za Rais Dkt Samia Suluhu Hassan katika kuwaletea maendeleo wananchi, amefanya safari nyingine ya kutoka Kasulu mpaka Tabora kuhamasisha utalii wa ndani.

Akizungumzia safari hiyo, Gadafi ambaye ni mwalimu mkuu wa shule ya msingi Junga iliyopo halmashauri ya mji wa Kasulu amesema, maamuzi ya kuibeba ajenda hiyo, yamechagizwa na mafanikio yaliyopatikana katika sekta ya utalii nchini baada ya Rais wa Jamhuri ya Muuungano wa Tanzania Dkt Samia Suluhu Hassan kuuhamasisha umma na dunia kwa ujumla kuhusu fursa za utalii zilizopo nchini.

Gadafi aliyeipa safari hiyo jina la “utalii wa magharibi”, anatarajia kuikamilisha mwishoni mwa wiki kwa kupita katika maeneo mbalimbali ya utalii na uhifadhi yaliyopo kwenye mikoa ya Tabora na Kigoma ambako pia atakuwa anazungumza na viongozi mbalimbali wa maeneo hayo.

Sanjari na utalii huo,  malengo mengine ya “safari ya magharibi” ni kuwahamasisha wananchi kushiriki katika uchaguzi mkuu wa Rais, wabunge na madiwani utakaofanyika Oktoba mwaka huu, kuilinda amani ya Tanzania na uzingatifu katika utunzaji wa afya kwa makundi maalumu hususan watoto, kina mama na watu wenye ulemavu.

Gadafi ambaye katika siku za karibuni amejipatia umaarufu mkubwa kutokana na kutumia usafiri wa baiskeli kwenda maeneo mbalimbali ya nchi akiwa amebeba bendera ya halmashauri ya mji wa Kasulu na ajenda za kitaifa, amedhamiria kuendelea na utaratibu huo ili kuyafikia maeneo mengi zaidi.

 

Post a Comment

Previous Post Next Post