Na Mapuli Kitina Misalaba
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Shinyanga, Kamishna
Msaidizi Mwandamizi wa Polisi (SACP) Janeth Magomi, amewatakia heri ya sikukuu
ya Pasaka wakristo na wananchi wote wa Mkoa wa Shinyanga, huku akibainisha kuwa
jeshi la polisi limejipanga kikamilifu kuhakikisha amani na usalama vinatawala
katika kipindi chote cha maadhimisho ya sikukuu hiyo takatifu.
Akizungumza na Misalaba Media leo Jumamosi Aprili 19, 2025, Kamanda
Magomi amesema jeshi lake limeimarisha ulinzi katika maeneo yote muhimu ikiwemo
makanisa, barabarani na katika maeneo ya burudani, ili kuhakikisha wakazi wa
Shinyanga wanaadhimisha Pasaka kwa amani na utulivu.
Ameeleza kuwa mikakati madhubuti ya kiusalama
imeandaliwa na kutekelezwa katika Halmashauri zote sita za Mkoa wa Shinyanga,
ambazo ni Manispaa ya Shinyanga, Halmashauri ya Wilaya ya Shinyanga, Kishapu,
Ushetu, Kahama na Msalala, ikiwa ni pamoja na kuhakikisha askari wapo tayari
muda wote kuhakikisha hakuna uvunjifu wa amani.
“Tumejipanga
vizuri kuhakikisha kwamba tunasimamia na kuimarisha shughuli zote za ulinzi na
usalama kuanzia mkesha wa Pasaka leo Jumamosi. Katika makanisa yote tumejipanga
vizuri, na hilo ni jukumu letu la msingi,” amesema.
Kamanda huyo amewaasa wazazi na walezi kuhakikisha
watoto wao wapo salama wakati wa kusherehekea Pasaka, akisisitiza marufuku ya
disko toto, ambayo mara nyingi huwa chanzo cha madhara kwa watoto.
“Nisisitize
kwamba disko toto hapana, nimepiga marufuku. Watoto kama ni kanisani waende,
lakini wazazi wanaweza kuwaambatana na watoto kuwapeleka kwenye sehemu nzuri za
kubembea au kupumzika wakiwa pamoja, ili kuhakikisha usalama wao,”
amesema.
Aidha, Kamanda Magomi ametoa wito kwa madereva wa
vyombo vya moto, hususan bodaboda, waendesha guta, pamoja na watembea kwa
miguu, kuheshimu sheria za usalama barabarani ambapo ameonya kuwa jeshi la
polisi halitasita kuchukua hatua kali kwa wote watakaokiuka sheria, hasa wale
watakaokuwa wakitumia vilevi wakati wa kuendesha vyombo vya moto.
“Sisi
tupo barabarani masaa 24 kuhakikisha hawatumii vilevi wakati wa kuendesha
vyombo vya moto. Tunataka sherehe hizi zisherehekewe kwa amani na utulivu,”
amesisitiza.
Mwisho, Kamanda Magomi amewashukuru wananchi wa Mkoa
wa Shinyanga kwa ushirikiano wanaoutoa kwa jeshi la polisi, na kuwatakia Pasaka
njema.
“Nawashukuru
sana wananchi wote wa Mkoa wa Shinyanga kwa ushirikiano mkubwa wanaolipa jeshi
la polisi katika kuhakikisha kwamba amani na utulivu vinatawala. Nawatakieni
nyote Pasaka njema, na Mungu awabariki sana.”
Post a Comment