" KIJANA WA MIAKA 16 AJINYONGA KATIKA KIJIJI CHA MWANG'OSHA, KAMANDA WA POLISI SHINYANGA SACP MAGOMI ALAANI VITENDO VYA KUJITOA UHAI

KIJANA WA MIAKA 16 AJINYONGA KATIKA KIJIJI CHA MWANG'OSHA, KAMANDA WA POLISI SHINYANGA SACP MAGOMI ALAANI VITENDO VYA KUJITOA UHAI

Na Mapuli Kitina Misalaba

Kijana mwenye umri wa miaka 16 anayefahamika kwa jina la Kulwa Yusuph Bukulu amefariki dunia kwa kujinyonga katika kijiji cha Mwang’osha, kata ya Nyamalogo, Halmashauri ya Wilaya ya Shinyanga.

Tukio hilo limetokea Aprili 11, 2025 majira ya saa nne asubuhi, ambapo taarifa zake zimethibitishwa na Mwenyekiti wa kijiji cha Mwang’osha, Magina Lugembe, alipokuwa akizungumza na Misalaba Media.

“Baada ya kupata taarifa za tukio hili nilifika eneo la tukio na kukuta kweli kijana huyo amejinyonga. Niliwajulisha viongozi mbalimbali wakiwemo askari wa jeshi la polisi ambao walifika eneo hilo na kuanza uchunguzi,” amesema Lugembe na kufafanua kuwa marehemu alikuwa akiishi kwa ndugu yake kijijini hapo.

Akizungumza kuhusu tukio hilo, Kamanda wa Polisi Mkoa wa Shinyanga, Kamishna Msaidizi Mwandamizi wa Polisi (SACP) Janeth Magomi, amethibitisha kutokea kwa kifo hicho na kueleza mazingira ya tukio.

“Ni kweli, tulipokea taarifa za kijana aitwaye Kulwa Yusuph Bukulu kuwa amejinyonga hadi kufa. Jeshi la polisi lilifika eneo la tukio na kukuta marehemu amejinyonga kwa kutumia kamba iliyofungwa kwenye kenchi ya stoo ya pumba za mifugo,” amesema SACP Magomi.

Ameongeza kuwa baada ya taratibu zote za uchunguzi wa kitabibu kukamilika, mwili wa marehemu ulikabidhiwa kwa ndugu zake kwa ajili ya maziko yaliyofanyika Aprili 13, 2025.

Kamanda Magomi ametoa wito kwa jamii kuendelea kushirikiana na jeshi la polisi katika kutoa elimu ya kujitambua kwa vijana.

“Ni tukio la kusikitisha sana. Kwa haraka unaweza kuona kijana huyu alikuwa amekata tamaa. Tunaendelea kutoa elimu kupitia polisi jamii na viongozi wa dini kwa imani zao tofauti kuhimiza watu kutorudi nyuma au kujitoa uhai wao pindi wanapopitia changamoto. Siyo sahihi kujinyonga kwa sababu ya kukata tamaa,” amesema SACP Magomi.

Jeshi la polisi limeeleza kuwa lingeweza kumchukulia hatua kijana huyo kwa kosa la kujaribu kujiua iwapo angekuwa hai, na hivyo limehimiza jamii kuwa makini na matukio ya aina hiyo ili kuokoa maisha ya vijana.


Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Shinyanga, SACP Janeth Magomi akizungumza.

 

Post a Comment

Previous Post Next Post