" KISWAHILI NI KIUNGO MUHIMU CHA MAENDELEO YA JUMUIYA YA AFRIKA MASHARIKI

KISWAHILI NI KIUNGO MUHIMU CHA MAENDELEO YA JUMUIYA YA AFRIKA MASHARIKI

 Na: Calvin Gwabara 

Vijana kama nguvu kazi ya maendeleo ya Jumuiya ya Afrika Mashariki wametakiwa kujifunza, kuipenda na kuisambaza lugha ya Kiswahili ili kuifanya jumuiya hiyo kuwa imara na kudumisha umoja kwa nchi zote.


Mhadhiri mwandamizi na Mkuu wa Idara ya Taaluma za lugha kutoka Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo SUA Dkt. Onesmo Nyinondi akiwa ameshika cheti cheke pongezi kwa kushiriki Kongamano hilo na kuwasilisha mada.


Wito huo umetolewa na Mhadhiri mwandamizi na Mkuu wa Idara ya Taaluma za lugha kutoka Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo SUA Dkt. Onesmo Nyinondi wakiti akitoa wasilisho lake kwenye kongamano la kwanza la kimataifa la Kiswahili lililofanyika kwenye uwanja wa taifa wa sherehe za uhuru Kololo Kampala nchini Uganda.

 “Vijana ukisikiliza wimbo wetu wa Jumuiya ya afrika mashariki unazungumzia umoja wetu ndio nguzo yetu lakini ili tuweze kufikia lengo hilo ni lazima tuwe na lugha moja inayotuunganisha wanajumuiya yote ya afrika mashariki ili mtu anapotoka eneo moja kwenda kwingine kufanya biashara au kutafuta maisha aweze kuelewana kwa lugha moja na sisi lugha yetu ni Kiswahili” alifafanua Dkt. Nyinondi.

Aliongeza “ Umoja tunaouimba unatoka wapi kama mtu akitoka Guru kwenda Mbarara haelewani lugha na watu wa pale na akitoka Mbarara kwenda DRC kongo au Kenya hawezi kuwasiliana? Swala la Kiswahili linahitaji msukumo wa kipekee ili kifahamike na kutumiwa na watu wote ndani ya jumuiya yetu”.

Akitolea mfano maneno kwenye kitabu cha mwanzo 11 msatari ule wasita kuhusu waliotaka kujenga mnara wa babeli na baada ya Mungu kuona watu wale kwa umoja wao wanaweza kweli kufika mbinguni aliwabadilishia lugha na hivyo kuwafanya washindwe kuelewana na hatimae ujenzi wa mnara wa babeli ukakwama.

Dkt. Onesmo amesema umoja na maendeleo ya Jumiya ya Afrika ya Mashariki yanawahitaji vijana ambao wanaongea  lugha moja ya Kiswahili vizuri katika shughuli mbalimbali ili kuondoa kikwazo cha lugha kwenye masuala ya mashirikiano baina yao.

Aidha amependekeza kuwepo na vitabu vidogovidogo ambavyo vinaeleza kwa Kiswahili mambo mbalimbali ya makabila yaliyo ndani ya jumuia hiyo ili kila mmoja aweze kuelewa pamoja na vitabu vyene istilahi zake kwenye shughuli mbalimbali za maendeleo.

Pia amependekeza kuwe na wiki ya Kiswahili ili kuongeza uelewa kwa jamii kwenye jumuiya yote na kuona kuwa pamoja na mipaka ya afrika mashariki lakini Kiswahili kiwe kiunganishi kikubwa cha watu ndani ya jumuiya nzima.

Mhadhiri huyo kutoka SUA amesema mapinduzi ya jambo lolote huanza na mtu mmoja na kisha kikundi na baadae jamii nzima hivyo kila mmoja aanze kufikiria umuhimu wa lugha ya Kiswahili kwa maendeleo ya watu maana penye nia pana njia.

Akitoa wasilisho lake liliohudhuriwa na Balozi wa Tanzania nchini Uganda na Balozi wa Uganda nchini Tanzania sambamba wawasilishaji wengine akiwemo Prof. PLO Lumbumba, Prof A.  Mtembei, Prof Wala na maguru wengine wa Kiswahili duniani na kushirikisha watu wengine mbalimbali zaidi ya 8000 wakiwemo Wanasiasa, Maafisa wa serikali, mabalozi, wasimamizi kutoka vyuoni, walimu, wanafunzi

Kongamano hilo lilihusisha washiriki kutoka nchi za Uganda, Tanzania, Kenya, Somalia, South Sudan, DRC, Rwanda, Burundi, Ghana, Nigeria and Canada.


Mhadhiri Mwandamizi na Mkuu wa Idara ya Taaluma za lugha kutoka Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo SUA Dkt. Onesmo Nyinondi (Wa pili kushoto) akiwa na maguru wengine wa kiswahili kwenye picha ya pamoja akiwemo Prof. PLO Lumumba.




Post a Comment

Previous Post Next Post